May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Serikali yaombwa kuunga mkono harakati za kumkomboa msichana

Na Mwandishi wetu, timesmajira

SHIRIKA lisilo la Kiserikali la Msichana Initiative limeiomba Serikali kurishika mkono katika harakati za kumkomboa mtoto wa kike na kutambua haki zao na kupinga ukatili wa kijinsia.

Hayo yamebainishwa leo Februari 23Jijini Dar es Salaam na Msimamizi Mradi wa Sauti YetuNguvu Yetu, Rosemary Richard katika mafunzo yaliyojumuisha viongozi wasichana 20 kutoka mikoa minne kupitia mradi huo yenye lengo namna kuwawezesha kubeba ajenda zao na kuzipigania.

Amesema mradi wa sauti yetu nguvu yetu umelenga kutengeneza jukwaa la wasichana kwa kuwakutanisha na kutambua ajenda zao na kuimarisha nguvu ya pamoja.

“Lengo la kukutana na wasichana hawa ni kupeana mafunzo, na mikakati ya namna gani wasichana hawa wanapokwenda kutekeleza majukumu yao huku wakiwa wamebeba ajenda mbalimbali ikiwemo kupinga ndoa za utotoni, kuamasisha usawa wa kijinsia sambamba na kuwawezesha ili waweze kuwa chachu ya uongozi,”amesema Rosemary.

Amesema mradi wa sauti yetu nguvu yetu ni wa miaka miwili ambao umeanza mwaka 2023 na unatarajia kumalizika octoba 2024.

Aidha amesema mradi huo umewafikia viongozi wasichana 20 kutoka katika mikoa minne ikiwemo mkoa wa Pwani unaohusisha wilaya ya bagamoyo, Tabora wilaya nzega, Dodoma wilaya ya kongwa pamoja na Dar es salaam.

“Kupitia viongozi hawa wasichana 20 kutoka katika mradi huu wa sauti yetu wameweza kuunda vikundi ambavyo vimefikia wasichana 240,”amesema

Vilevile amesema katika uendelevu wa mradi wamekuwa wakitoa mafunzo mbalimbali kwa wasichana hao huku wakijikita zaidi katika dhana nzima ya uhanaharakati pamoja na mambo ya uongozi.

Naye Kiongozi wa Msichana Kutoka Mkoa wa Pwani Wilaya ya Bagamoyo, Leonardina Sosthenes amesema katika mkoa huo kumekuwa na wimbi kubwa la ndoa za utoto ambapo chanzo kikubwa ni tamaa za mali na kukosekana kwa elimu ya ukatili kwa watoto.

Amesema kupita shirika hilo wameweza kuokoa watoto watatu ambao waliingia kwenye ndoa na kufanikiwa kurudi shule.

“Suala la ndoa za utotoni limekuwa changamoto sana katika mkoa wetu tumeokoa watoto wa tatu ambao waliolewa wenye umri mdogo na tumewarudisha shule kuna mmoja yeye alikuwa mjamzito tulimsaidia akafanya mitihani ya darasa la saba,amejifungua Disemba na sasa yupo kidato cha kwanza,”amesema Leonardina.

Naye,msichana kiongozi Kutoka Wilaya ya Ubungo, Mwajuma Hima ametoa rai kwa wazazi kuwa karibu na watoto na kutokuwaamini ndugu na kuwaachia watoto kwani wamekuwa wakichangia kwa kiasi kikubwa ukatili kwa watoto.