Na Doreen Aloyce,Timesmajira online, Dodoma
Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini Michael Mwakamo amesema licha ya serikali kuendelea kuboresha huduma za afya hapa nchini kuna haja ya kuweka mikakati ya kuboresha bima ya afya kwa wote jambo ambalo litasaidia wananchi kupata matibabu kwa urahisi.
Kauli hiyo ameitoa viwanja vya Bunge jijini Dodoma wakati alipokuwa akifanya mahojiano na waandishi wa habari juu ya bajeti ya Wizara ya afya kwa mwaka 2023/2024 ambayo imepitishwa.
“Tunaona kazi ya vituo vya afya ilivyo kubwa ujenzi wa zahanati vijijini, namna ya usambazaji wa vifaa vya kutolea huduma za afya zinakwenda mpaka ngazi za chini hii inaleta matumaini makubwa lakini niombe serikali ikazie suala la bima kwa wote ili wananchi wapate huduma stahiki,”amesema Mwakamo.
Pia amesema utoaji wa vifaa tiba kwenye maeneo ya vijijini kunarahisha na kupunguza ongezeko kubwa la mama wanaojifungulia nyumbani na vifo vya uzazi vinapungua.
Aidha amesema ndani ya jimbo lake bado kuna changamoto ya kukosekana kwa dawa kwenye vituo vya afya jambo ambalo serikali wanalitengenezea ya kuwa na bima ya afya kwa wote .
Hata hivyo ametoa wito kwa watanzania kutoa ushirikiano kwa Rais Samia Suluhu Hassani ili zile juhudi alizonazo aweze kufanya mengi huku akiwataka wananchi wa jimbo lake kuendelea kuunga harakati za kuwapambania na hatawaangusha.
“Niko karibu na wananchi wangu wa Kibaha Vijijini nawaahidi sitawaangusha nipo Bungeni kuwapambania kumalizia zile changamoto ndogo ndogo zilizopo hususani barabara na maji,” amesema Mbunge Mwakamo.
More Stories
Maadhimisho siku ya nyuki Duniani ni fursa adhimu kiuchumi
NMB ‘yafunga ndoa’ na wanawake wanaomiliki shule, vyuo Tanzania
RC Mwanza afanya ziara ya kikazi katika mradi wa uwekezaji jengo la Hotel ya nyota tano wa NSSF