May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Sangu aomba miradi ya maji itekelezwe kwa hati fungani

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online, Dodoma

MBUNGE wa Kwela Deus Sangu ameishauri Wizara ya Maji kutumia njia ya hati fungani ya Kijani kama walivyofanya Mamlaka ya Maji ya Tanga (TANGAUWASA) ili kupata chanzo cha fedha madhubuti kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji nchini.

Aidha ameiomba wizara hiyo kulipa madeni ya wakandarasi wanaotekeleza miradi ya maji katika Jimbo la Kwela na kuwezesha usafiri ofisi ya Meneja wa Maji wilaya ili kurahisisha shughuli za kuwapatia maji wananchi wa Kwela.

Sangu ameyasema hayo Bunge Mei 9 wakati akichangia bajeti ya wizara ya Maji  kwa mwaka 2024/2025 .

Amesema mara nyingi wabunge wamekuwa wakipiga kelele bungeni kuhusu miradi ya maji kutofanya vizuri wakati nchi hii haina shida ila inahitaji fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji  kwa maana ya huduma hiyo iwafikie wananchi.

“Tuna maji ya chini  ‘surface water’ lakini ni namna gani tutayatoa yawafike wananchi ndiyo jambo linaloumiza vichwa kama Taifa,lakini katika hotuba yako umeonesha umakini ulipoongelea  habari ya hati fungani ya kijani ya Tangauwasa ,na umeona Tangauwasa ilivyofanya vizuri ,ukaicjukulia mfano lakini   ni wazi ndiyo taasisi ya kwanza Barani Afrika kutoa hati fungani ya kijani, 

“Sasa huo ndiyo mwelekeo wa kutafuta njia nyingine ya fedha kwenye  miradi ya maji ,tuking’ang’ania vyanzo vya water fund ,e4R ,sijui fedha kutoka serikalini tutapiga hatutaenda mbele.”amesema Sangu

Ametumia nafasi hiyo kuwapongeza wadau wote waliofanikksha mchakato wa hati fungani ya TANGAUWASA wakiwemo  

  United National Capital Devwlopment Fund ( UNCDF)  ambao ndiyo waliosaidia katika michakato ya kuwezesha katika hatua zote mpaka hati fungani ya kijani ikaingia kwenye soko na hadi sasa tumefikia hatua nzuri.

Vile vile amwapongeza  Tanzania Capital Market  and security Authority (CMSA) kwa kusapoti mchakato huo,soko la hisa la Dar es Salaam ambao wamekuwa wakitoa ushauri mzuri pamoja na benki ya NBC ambao wanasimamia hati fungani hiyo  wizara ya fedha pamoja na waziri wa Maji.

“Tulikuwa tuna mpango wa kupata shilingi  bilioni 53.1 lakini ndani ya muda tulioweka hii bondi tumepata shilingi  bilioni 54.7 ,yaan tumezidi  lengo kwa asilimia 103,kwa hiyo huu ndo uwe mwanzo kwenye uwekezaji kwenye  sekta ya maji .”amesisitiza Sangu na kuongeza kuwa 

“Hati fungani ya kijani ni bondi inayotolewa kwa ajili ya mazingira, na dunia uelekeo wake ni kwenye  utunzaji wa mazingira ,Sasa leo hii una mamlaka sita zenye category  ya daraja la A,tuna hiyo Tanga imeshaondoka  ambayo sasa inaenda kuwezesha kwenye mradi mkubwa wa maji mkoa wa Tangu na mikoa ya jirani,

“Lakini kuna mamlaka ya Maji Moshi nayo iende kwenye  uelekeo huo tukitoka hapo Mamlaka ya Maji ya Dar es Salaam ambayo najua wanataka waingie na bondi ya shilingi  bilioni 200,tuombe mheshimiwa Waziri kama tulivyofanya Tangauwasa nao hawa tuende kwa njia hiyo,

“Mamlaka ya Maji Kahama nao wapo vizuri wanaweza wakaingia kwenye mfumo huo Mamlaka ya maji Iringa nao wapo katika Category hii ,na Mamlaka ya Maji Mwanza  zote hizi tutapunguza mzigo wa kugombaniana shilingi bilioni 60 zilizotolewa na Rais Dkt.Samia Samia Suluhu Hassan  kwa ajili ya kwenda  kulipa madeni lakini tunagombaniana .”amesema Mbunge huyo

Amesema kukiwa na  vyanzo vya fedha wabunge wataondokana kugombania chanzo kimoja cha fedha na tutakuwa na vyanzo vingi badala ya kutegemea fedha kutoka kwenye mfuko mkubwa wa hazina.

“Naomba Waziri usisitize kwenye hayo maeneo (mikoa) ili tuondokane na changamoto ya utekelezaji miradi ya maji nchini badala ya kukariri chanzo kimoja tu ambacho tunagombaniana.”amesema

Kuhusu kuoatiwa usafi ofisi wa Meneja wa Maji wa wilaya amemuomba Waziri wa Maji Jumaa Aweso aliangalie hilo na kulifanikisha.

Kuhusu madeni ya wakandarasi wanaofanya miradi ya maji katika jimbo la Kwela Sangu ameiomba serikali iwalipe wakandarasi madeni hayo ili kazi za ujenzi wa miradi ya maji jimboni humo iweze kuendelea.

“Kuna bwawa la Kwela ambalo ni mradi wa shilingi bilioni 6,lakini mkandarasi anadai shilingi bilioni  2,mwaka mzima sasa amesimama kazi ,naomba katika bilioni 60 uliyopewa, shilingi bilioni  2 hizi tuletee Kwela ili mradi wa Kwela ukamilike ,

“Lakini pia  mradi wa Kaoze Group,yule mtu mmempa kazi ameenda kuchukua ‘advance payment bond’ kama ‘security’ lakini hamjampa hela malipo ya awali ya shilingi bilioni 300,Kaoze group imesimama hakuna kinachoendelea,

“Lakini pia Mamlaka ya Maji katika mji mdogo wa Laela mmeanza mchakato mnataka muifanye Laela iwe na Mamlaka ya maji ya mji mdogo wa Laela ambayo itaweza sasa kuwa na watumishi wa kudumu na kuendesha mambo yake kama Mamlaka ya Maji ,niombe hili jambo ulisukume na ukifanya hayo kuna mambo mengi nitakuandikia kwa maandishi yanayohusu kero ya maji jimbo la Kwela na mkoa wa Rukwa tukiwa na ajenda ya ziwa Tanganyika.”amesisitiza Sangu