May 15, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Salim: Waandishi wa habari someni sheria zinazohusu habari

Na Jackline Martin, TimesMajira Online

Waandishi wa habari nchini wametakiwa kusoma sheria zinazohusu masuala ya habari na nyingine ili wanapotaka zirekebishwe wawe na ushawishi mkubwa kwa watunga sheria na jamii.

Hayo ameyasema Mjumbe wa Kamati Tendaji ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Salim Said Salim wakati akifungua warsha ya kuwajengea uwezo wahariri juu ya mipango ya uchechemuzi wa mabdiliko ya sheria za habari.

Salim amesema kuwa mwandishi wa habari akijua haki zake, sheria zinazoongoza tasnia ya habari ataweza kukutana na makundi mbalimbali ya jamii ikiwemo wabunge na kuwashawishi juu ya sheria zinaminya uhuru wa habari na haki za binadamu.

“Bado waandishi hatujawa na uelewa mpana wa sheria zinazotuhusu, tufanye jitihada kuzijua. Tuwashawishi wenzetu juu ya sheria zinazokwaza ukuaji wa tasnia ya habari na maendeleo ya Taifa”

Naye Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile, amesema wataendelea kuwa mstari wa mbele kupigania mabadiliko ya sheria zinazogusa tasnia ya habari kwa kushirikiana na wadau wengine.Kwa upande wake Walace Maugo, aliwataka waandishi wa habari nchini kupigania haki za Watanzania na kuboresha maisha yao kupitia taaluma yao na kazi wanazozifanya kila siku.

“Kama tunavyofahamu kwamba sisi ndiyo tunaotengeneza mijadala kwenye jamii, kazi yetu kubwa ni kuhakikisha maisha bora yanapatikana na watu wanafurahia maisha katika nchi yao, tusijione wanyonge kuna hatua kubwa zimechukuliwa kutokana na kazi tunazozifanya,” alisema Maugo