May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia apongezwa kwa kudumisha amani nchini

Na Allan Vicent, TimesMajira Online, Tabora

KANISA la Tanzania Assemblies of God-Kitete Christian Centre (KCC) la mjini Tabora limempongeza Rais wa awamu ya 6 Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kudumisha amani, utulivu na mshikamano wa Watanzania wote.

Akitoa salamu za krismas katika ibada iliyofanyika jana kanisani hapo Askofu Mstaafu wa Kanisa la TAG Jimbo la Tabora ambaye pia ni Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la KCC, Rev.Paul Meivukie amesema amani, utulivu na mshikamano uliopo nchini ni matokeo ya uongozi mzuri wa Rais Samia.

Amebainisha kuwa Rais Samia ni Kiongozi mvumilivu, asiyependa kusema haraka, na hata linapotokea jambo lolote hutuliza akili kwanza kabla ya kutoa tamko, hekima hii ndiyo imefanya amani na utulivu kuendelea kuwepo nchini.

‘Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais, tunaomba Mungu aendelee kumbariki na kumuinua zaidi katika utumishi wake ili yale mazuri yote aliyoyakusudia yaweze kutimia na kunufaisha wananchi,’ alisema.

Rev. Meivukie ameongeza kuwa katika kuadhimisha sikukuu hii ya kuzaliwa kwa Yesu Kristu, Mfalme wa amani, wanamwomba Mungu aendelea kumwonekania na kumfungulia amani, baraka na ushindi katika kila alifanyalo.

Amewashukuru waumini wote wa kanisa hilo kuwa kwa mshikamano mzuri katika utumishi wa Mungu na kuwataka kuendelea kumwomba Mungu ili Yesu Kristu, Mfalme wa Amani aendelee kutamalakia katika taifa la Tanzania.

Akinukuu maandiko matakatifu katika kitabu cha injili ya Mathayo 21:12-13 na Marko 11:15-17 amewataka wakristo na jamii kwa ujumla kumruhusu Yesu Kristo atawale maisha yao na kuachana na mambo yasiyofaa.

Wakizungumza na gazeti hili baadhi ya waumini wa kanisa hilo wamemshukuru Mungu kwa kuadhimisha sikukuu hiyo kwa amani na utulivu na kuongeza kuwa krismas sio kula na kunywa tu bali kutafakari maisha yao na kumgeukia Mungu.

Mama Kisa Mwasulano ambaye ni Mwenyekiti wa Idara ya Wanawake (WWK) kanisani hapo ameshauri jamii kuadhimisha sikukuu hiyo kwa kumpa Yesu maisha yao ili azaliwe mioyoni mwao na kuwaongoza katika mapito yote.

Amesisitiza kuwa Yesu Kristo akiwa ndani ya mioyo yao wataishi kwa amani, furaha na upendo lakini kama hayuko ndani yao hawatakuwa salama kwa kuwa mioyo yao itajazwa na chuki, ugomvi na mifarakano.

Mwimbaji wa kwaya kuu ya kanisa hilo ya Uamsho, Yusuph Joseph ameitaka jamii kuadhimisha sikukuu hiyo kwa amani na utulivu ili kuunga mkono dhamira njema ya Mheshimiwa Rais ya kuwa na taifa lenye amani, utulivu na mshikamano.

Aidha ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kumwombea ili Mungu ampe hekima na kumwongoza katika kila alifanyalo ili liwe na tija kubwa kwa maendeleo yao.

Askofu Mstaafu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG) Jimbo la Tabora ambaye pia ni Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Kitete Christian Centre ( KCC) la Mjini Tabora Rev Paul Meivukie akihubiri kwenye ibada ya Krismas kanisani hapo.