May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Prof.Kitila ashtushwa na kasi ya mto Gide kumomonyoa udongo na kuangusha Makazi


Na Mwandishi wetu, timesmajira

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji na Mbunge wa Jimbo la Ubungo Prof. Kitila Mkumbo ameahidi kuwa Serikali itachukua hatua madhubuti kuzuia mmomonyoko wa udongo unaokula makazi kutokana na kuhama kwa mito mkoani Dar es Salaam.

Akiwa ziarani katika Kata ya Ubungo Prof. Kitila Mkumbo amejionea athari za mafuriko kwenye mto Gide na kushuhudia baadhi ya makazi yakiwa yamesombwa na maji huku nyumba nyingine zikiwa hatarini kusombwa na maji likiwemo mojawapo ya majengo katika Hoteli maarufu ya Land Mark.

“Huu mmomonyoko namna unavyokwenda kwa kasi unatishia kutoweka kwa makazi mengi na hili jambo ni kubwa kuliko unavyoweza kufikiria, ipo haja ya kuchukua hatua kubwa zaidi”Amesema Prof. Kitila Mkumbo.

Amesema namna athari zilivyo kwa mvua hizi za El-nino ni dhahiri kunapaswa kuwepo na hatua za dharula, za muda mfupi, mrefu na wa Kati na muda mrefu maana maji yanakuja kwa kasi kubwa.

Katika ziara hiyo Prof. Kitila ametembelea kivuko kinachotenganisha wakazi wa Ubungo Kisiwani na Ubungo Maziwa ambacho kimesombwa na maji na kuchukua hatua za dharula za kutafuta fedha kwaajili ya kujenga kivuko hicho kabla ya shule kufunguliwa January, 2024 ili kuwezesha wanafunzi na wananchi kupita bila shida.

Amewaagiza TARURA kufanya tathimini ya haraka na kuanza ujenzi mara watakapokabidhiwa fedha kiasi cha Sh. Milioni 90 kinachotakiwa kukamilisha ujenzi huo.

Katika hatua nyingine Mbunge huyo ameahidi kufanyiwa matengenezo ya dharula kwa baadhi ya barabara zilizoharibiwa na mvua pamoja na Vivuko huku akiwataka wananchi kuwa na subra wakati Serikali ikishughulikia changamoto zinazowakabili.