May 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Pinda:Amani na utulivu ndio msingi wa maendeleo ya nchi

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Dodoma

WAZIRI Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda ameiasa Jumuiya ya Maridhiano  Nchini kuendelea kulisemea suala la kudumisha amani na utulivu nchini kwani ndio msingi wa maendeleo ya nchi.

Pinda ameyasema hayo jijini hapa kwenye mkutano wa amani wa Jumuiya hiyo uliokuwa na lengo la kuipongeza Serikali ya awamu ya sita  inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuimarisha miradi ya kiuchumi na kuendeleza  miradi ya maendeleo.

Amesema amani iliyopo nchini ikiachwa ipotee kuirejesha tena siyo kazi rahisi kama watu wengine wanavyodhani huku akiisihi Jumuiya hiyo kujipanga ili kuepusha kupotea kwa amani kwa maslahi mapana ya watanzania na nchi kwa ujumla.

Vile vile amewaasa wananchi wote kuhakikisha ,kila mmoja kwa nafasi yake anadumisha amani na utulivu na kuwataka kujua amani ni tunu ambayo ikipotea kuirejesha ni gharama kubwa.

Aidha ameitaka Jumuiya hiyo kuhakikisha hakuna malumbano baina ya viongoiz wa dini kwani wao ndio kioo cha jamii katika masuala ya amani na utulivu huku akisema hawapaswi kuhitilafiana hadi wananchi wajue.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo Taifa Sheikh Dkt.Alhad Mussa Salum amempongeza Rais Samia kwa kuendelea kuhubiri amani na utlivu  nchini hali inayowawezesha watanzania kuendelea kufanya shughuli zao mbalimbali zikiwemo za kiuchumi bila bughudha yoyote.

Awali Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo  Israel Ole Gabriel amesema,Jumuiya ya Maridhiano ipo katika wilaya zote na mikoa 26 hapa nchini  huku kukiwa na viongozi wake katika Jumuiya hizo.

Aidha amesema lengo la mkutano huo ni kuipongeza Serikali ya awamu ya sita kwa kazi kubwa ambayo imeendelea kuifanya ya kudumisha amani na utulivu nchini.

Pia amesema lengo jingine la mkutano huo ni kuipongeza Serikali ya awamu ya sita inavyoendeleza miradi iliyoanzishwa tangu serikali ya wamu ya kwanza .