April 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Parimatch yaidhamini Mashujaa FC

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Zikiwa zimesalia takribani siku nane kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Kampuni ya michezo ya Kubahashiri Parimatch imetangaza rasmi kuingia makubaliano ya kuidhamini Klabu ya Mashujaa FC kwa msimu wa 2023/24.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Parimatch Tanzania, Erick Gerald wakati wa zoezi la utiaji sahihi wa mkataba ambao umefanyika leo katika ukumbi wa ofisi za Mashujaa fc baina ya Uongozi wa Kampuni hiyo mbele ya vyombo mbalimbali vya habari.

Aidha Erick amesema lengo mahususi ya mkataba huo ni kukuza soko la mpira nchini pamoja na kuimarisha ushirikiano baina ya pande zote mbili.

“Parimatch tumekuwa wadau wakubwa kwenye sekta ya michezo hapa nchini na nje ya nchi na kupitia udhamini huu unalenga kusaidia timu ambayo ina vijana wanaopata ajira, wanajenga afya na kuleta ushindani kwenye michezo”, amesisitiza Erick.

Kwa upande wake kiongozi wa timu ya Mashujaa FC, Benjamin Kisinda ameishukuru Kampuni ya Parimatch Tanzania kwa kuwaamini na kuwaunga mkono katika udhamini huo ambao utawasaidia kupunguza changamoto za uendeshaji wa klabu.

“Tunawashukuru wadhamini wetu Parimatch kwa kuja kuungana nasi katika kuendeleza soka, Mashujaa ni timu ambayo imepanda daraja msimu huu, kwa hivyo tunawakaribisha sana Kigoma katika familia ya Mashujaa”, amesisitiza Kisinda.