May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Nelsap yawezesha wanafunzi kufundishwa tehama

Na Penina Malundo, timesmajira

MRADI wa Kufua umeme wa maporomoko ya rusumo uliozinduliwa na program ya Nelsap umeweza kusaidia wanafunzi 20 wa Chuo cha Maendeleo cha Wananchi Ngara kilichopo mkoani Kagera ,kupata vifaa vya kujifunzia masomo ya Tehama ambayo yataweza kuwasaidia kujiajili au kuajiliwa baada ya kuhitimu masomo hayo.

Akizungumza hayo katika moja mahojiano na waandishi wa habari walipofika katika chuo hicho na kujionea namna ambavyo chuo kimeweza kuafaidika na miradi mbalimbali inayotolewa na programu ya Nelsap ,Mratibu wa Mafunzo wa Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Ngara,Mratibu Amoni Julus amesema msaada huo umeweza kuwapa faida kubwa kwa vijana wanaishi katika maeneo hayo na jirani kuweza kujiunga na chuo hicho na kuweza kusoma.

Amesema kwa mwaka 2023,chuo hicho kilibahatika kupata takribani wanafunzi 20 ambao wanapata mafunzo hayo katika chuo hicho ukilinganisha na miaka 2019/2020 ambao walikuwa watano huku wakiume akiwa mmoja na wanawake wanne.

”Tunaishukuru Nelsap kwa manufaa ambayo yamepatikana kwa shule yetu na hii imetokana na mradi wa nelsap kwa kutuwezesha vifaa vya kujifunzia kwani miaka ya nyuma tuliokuwa hatuwezi kufika idadi hii,”amesema na kuongeza

”Idadi hii inaridhisha kwa kiasi kikubwa utaona watoto wa kike ndio wamekuwa wengi kuja kusoma masomo haya hivyo yanachangia kwa nafasi kubwa ya wao kuja kuajiliwa au kujiajili ambapo itasaidia kupunguza utegemezi,”amesema.

Kwa Upande wake Mratibu wa Miradi ya Kimaendeleo inayosimamiwa na Program ya Nelsap upande wa Tanzania,Irene Chalamila amesema wamekuwa na miradi mingi ya kijamii wanayoifanya chini ya program ya Nelsap lengo ikiwa ni kuboresha maisha ya wananchi katika eneo hilo lenye Mradi mkubwa wa umeme wa maporomoko ya Rusumo ambapo unatazamiwa kuzinufaisha nchi tatu jirani ambazo ni Rwanda,Tanzania na Burundi.

”Ipo miradi mbalimbali ambayo imetekelezwa na Nelsap miongoni mwa miradi hiyo ni pamoja na utoaji wa Kompyuta ambayo zimewezesha wanafunzi kujifunza kwa vitendo masomo ya tehama wa Chuo cha Maendeleo cha Wananchi Ngara,Uboreshaji wa majengo ya kujifunzia ikiwemo jengo la ufundi selemara na uwashi,”amesema.

Amesema lengo kubwa la mradi huo wa Nelsap ni kuona ni namna gani maisha ya wananchi wanaboreka na wananufaika na mradi huo mkubwa wa umeme wa rusumo ambapo imeweza kutekelezwa kwa awamu ya kwanza na ya pili ya mradi.

Amesema kwa awamu ya kwanza ya mradi huo umeweza kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa kituo cha Afya ya rusumo ,ujenzi wa shule ya sekondari Mbalimbali ,Madarasa na Maabara ,pamoja na ujenzi wa madarasa pamoja na mradi wa kujenga na kuboreshaji mabweni ya Sekondari Rusumo.

Naye Mmoja wa wanufaikaji wa mradi huo katika Chuo hicho,ambaye ni Mwanafunzi wa masomo ya Tehama ,Teknolojia ya habari na Mahusiano,Steve John, ameushukuru mradi huo kuwepo katika eneo lao kwani wameweza kunufaika kwa mambo mengi ikiwemo kufahamu masuala ya tehama na kuona umuhimu wa kusoma tehama katika ulimwengu huu wa sasa.

Amesema alimaliza shule 2020 alikuwa mtaani hivyo alishawishika kusoma masomo hayo ya tehema na mpaka sasa ameweza kunufaika ambapo anaweza kujiajili au kuweza kuajiliwa kwani ni moja ya fani inayokuja kwa kasi duniani.

”Nawashukuru waliotupa msaada huu katika kuhakikisha sisi vijana tunafikia malengo yetu ya tehama au katika teknolojia ya habari tunashukuru sana,tunaomba kuendelea kutushika mikono kwani vijana bado ni wengi wanaotamani kuja kusoma masomo haya,”amesema.