April 24, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ndejembi awataka viongozi kusimamia kikamilifu ujenzi sekondari ya Kwemkabala

Na Veronica Mwafisi,TimesMajira Online,Muheza

NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Deogratius Ndejembi amewaelekeza Viongozi wa Wilaya ya Muheza mkoani Tanga, kuhakikisha wanasimamia kikamilifu ujenzi wa Shule ya Sekondari Kwemkabala unaogharimu shilingi milioni 66 zilizotolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) baada ya kutoridhika na maendeleo ya ujenzi huo.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akitoa maelekezo baada ya kukagua ujenzi wa madarasa katika Shule ya Sekondari Kwamkabala Wilayani Muheza, jijini Tanga ambao unajengwa kwa kutumia fedha za TASAF wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF katika Wilaya ya Muheza

Ndejembi ametoa maelekezo hayo baada ya kukagua ujenzi wa shule hiyo akiwa kwenye ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF katika Wilaya ya Muheza.

Akizungumza baada ya kukagua ujenzi wa Shule hiyo,Ndejembi amesema, kiasi cha fedha kilichotumika mpaka sasa hakiendani na kazi iliyofanyika na hii inatokana na ushauri au usimamizi mbaya uliotolewa juu ya ujenzi wa shule hiyo.

Walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wa Kata ya Genge Wilaya ya Muheza jijini Tanga wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani) wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF na kuhimiza matumizi mazuri ya ruzuku inayotolewa na TASAF kwa walengwa.

“Mhandisi anayesimamia ujenzi wa shule hii hakushauri vizuri kuanzia kwenye msingi mpaka ulipofikia, akiwa kama mtaalam, alitakiwa aangalie anachokishauri, kinachojengwa na thamani ya fedha iliyotolewa, hivyo Mkurugenzi na Watendaji wa TASAF muangalie namna gani ya kufanya ili jengo hili liweze kukamilika kwa ubora,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wa Kata ya Genge, Wilaya ya Muheza, jijini Tanga wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF na kuhimiza matumizi mazuri ya ruzuku inayotolewa na TASAF kwa walengwa.

Ndejembi ameongeza kuwa, kiasi cha fedha kilichobaki ambacho ni shilingi milioni 39 hakiwezi kukamilisha ujenzi wa shule hiyo kwa ubora kwani sehemu iliyobakia ni kubwa na fedha zilizobaki ni kidogo.

Ndejembi amesema Serikali imekuwa ikitoa fedha nyingi kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo, hivyo hafurahishwi kuona zikitumika vibaya.

Ujenzi wa shule hiyo unajumuisha vyumba viwili vya madarasa, ofisi na matundu matano ya vyoo.