April 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamati ikiwa kwenye Kiwanda cha Mzee Kisangani kinachotengeneza zana mbalimbali. Kutoka kushoto ni Mzee Kisangani, Prof. Madundo Mtambo, Prof. Silvester Mpanduji na Afisa Madini Mkoa wa Njombe Wilfred Machumu.Picha na Wizara ya Madini

‘Naona kama ndoto’- Mzee Kisangani

Issa Mtuwa – Njombe

Mjasiliamali mwenye umri wa miaka 60 asiejua Kusoma na Kuandika Rueben Mtitu maarufu kama Mzee Kisangani amesema, anaona kama ni ndoto kuona timu ya Wataalamu wa Wizara Nne kuja kwake kwa ajili ya kumsaidia, kwa lengo la kumsikiliza na kuweka mpango mkakati wa kumsaidia na kumuinua kutokana na udogo wa Kiwanda chake. Ubunifu wa kutengeneza kiwanda hicho kisicho na ubora wa Teknolojia ulipelekea Waziri wa Madini Doto Biteko kwenda kukitembelea na hatimae kuunda kamati hiyo.

Kauli hiyo, imesemwa na Mzee Kisangani leo Aprili 7, 2020 mkoani Njombe mara baada ya kamati kutembelea kiwanda chake na kujadiliana kuhusu changamoto zinazomkabili.

Kisangani amemshukuru Waziri wa Madini Doto Biteko kwa kutekeleza kila jambo aliloahidi kuhusu kiwanda chake ndo maana anashindwa kuamini macho yake. Biteko akiwa ziarani mkoani Njombe Machi 13-16, 2020 pamoja na mambo mengine alisema Wizara yake itamsaidia Mzee Kisangani kutokana na ubunifu wake na kwamba bidhaa zake zinatokana na Madini ya Chuma.

“Mpaka sasa alichosema Waziri Biteko kimetekelezwa tena kwa haraka. TANCOL wamesha niletea Mkaa wa Mawe, kikao na Wizara Nne walishakaa na matunda yake ni hii timu iliyofika na leseni kumi vimefanyika. Niseme nini zaidi ya kuishukuru serikali hii? Alisema Kisangani

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Prof. Silvester Mpanduji amesema, kamati yake imekutana na Kisangani na kujadili mambo mbalimbali katika maeneo yanayohusiana na biashara yake. Tumefurahi kuona ubunifu na uthubutu alionao na kweli ipo sababu ya serikali kumsaidia na kutatua changamoto zake ili mradi wake wa kiwanda kipanuke na kuongeza uzalishaji.

Prof. Mpanduji amesema, yale yote waliyoyabaini kupitia mradi wa Kisangani na namna ya kuyatatua yatawasilishwa kwa Waziri wa Madini Doto Biteko kupitia ripoti itakayowasilishwa. Ameongeza kuwa yapo mambo mengi waliyoyapitia na kwamba kamati itatoa mapendekezo kwa serikali kuona namna ya kumsaidia ili kiwanda chake kipanuke na kuongeza uzalishaji.

Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Prof. Madundo Mtambo amesema shabaha ya serikali kuwainuwa watu wenye ubunifu ni jambo zuri na nivyema kuwasaidia watu wanyonge wenye ubunifu kama Kisangani.

 Akizungumzia uzalishaji wa bidhaa zake sokoni, Mzee Kisangani amesema, achilia mbali ukosefu wa mtaji, makaa ya mawe, umeme na upanuzi wa kiwanda chake, soko na kuuzia bidhaa ni kubwa na hajawahi kukaa na bidhaa zilizokwisha tengenezwa.

Akizungumza mbele ya kamati, Andrea Chaula alisema Serikali ikimsaidia Kisangani watanufaika nao kwa sababu hata kabla ya kumuwezesha Mzee Kisangani ametoa ajira ya watu zaidi ya 30 na kwamba Serikali ikimpa nguvu uwezekano wa kuajiri watu wengi ni mkubwa kwa sababu kutakuwa na kazi nyingi za kufanya.

Asnat Mtitu ambae pia ni mjane amesema, anazidi kuiomba serikali kumsaidia Mzee Kisangani kwani hata wao wanaofanyakazi kwake wanapata kipato wanacholipwa na kuendesha maisha yao hivyo serikali isirudi nyuma katika kumsaidia.

Akiwa na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Biteko aliwaambia wajumbe wa kamati hiyo kuwa majuzi Gazeti moja liliandika kuhusu ongezeko la Mabilionea wapya kutoka Tanzania, hata hivyo alisema bado anataka kuona Mabilionea hao wakitokea kwenye sekta ya Madini. Hata hivyo wazo lake la kumsaidia Kisangani ili awe bilionea katika siku zijazo. 

Timu hiyo inaundwa na Wilfred Machumu (Tume ya Madini), Issa Mtuwa (Wizara ya Madini), Abbas Mruma (GST), Prof.  Silvester Mpanduji (SIDO), Prof. Madundo Mtambo Mkumbukwa (TIRDO), Dr. Yohana Mtoni (NDC),  Anorld Mapinduzi (NEMC), Leo Mavuka (TAMISEMI), na Dr. Hellen (Chuo Kikuu Mzumbe.