April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwandishi wa habari afariki baada  ya kujifungua

Na Esther Macha ,TimesnajiraOnline,Mbeya

CHAMA cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Mbeya(MBPC)kimepata pigo baada ya kuondokewa na mwanachama wake wa muda mrefu Hannerole Mrosso aliyefariki baada ya kujifungua katika Hospitali ya  Rufaa Kanda ya Mbeya kitengo cha Wazazi Meta Jijini Mbeya .

Akitoa taarifa mume wa marehemu Baraka Kasubiri ambaye ni Afisa Ustawi wa Jamii amesema mkewe alifanyiwa upasuaji na kujifungua mtoto wa kike na muda mfupi baada ya kujifungua alipoteza maisha.

Taratibu za mazishi zinafanywa eneo la Sokomatola Jijini Mbeya ambapo mwili utasafirishwa kwenda Namtumbo Mkoani Ruvuma kwa maziko yanayotarajiwa kufanyika jumapili Mei 15,2022.

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Mbeya Joseph Mwaisango amesema marehemu alikuwa ni mwanachama ambaye alikuwa na mchango mkubwa kwa tasnia ya habari pia alikuwa na ushirikiano na kila mtu.

Naye Mwenyekiti wa Jukwaa la Uchumi kwa wanahabari(MJEF) Kakuru Msimu amesema msiba huu umewaumiza hasa pale ambapo wanapompoteza mwenzao ambaye walitegemea kujikwakwamua kiuchumi.

Aidha Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wanahari wanawake Esther Macha amesema wamepata pigo kwani wamempoteza mwanachama wao ambaye alikuwa na mchango mkubwa tangu kuanzishwa chama chao.

“Chama chetu kimepata pigo kubwa kwani huyu sasa ni mwandishi wa habari wa kike wa pili kufarika katika chama chetu ,kwani hivi karibuni tulimpoteza mwanachama mwingine Johari Shani ambaye alipata ajali  mkoani Mwanza akiwa kwenye shughuli zake za kikazi ,kiukweli tumepoteza nguvu kazi kwenye Tansia ya habari”amesema Mwenyekiti huyo.

Martha Sambo amesema marehemu ambaye pia alikuwa mwanachama chama cha kusaidiana wanahabari(Amani) amefariki wakati chama chao kikiwa kichanga na marehemu alikuwa mshiriki mwaminifu.

“Ni vigumu kuamini kuwa Hannerole ametuacha kwani upole wake na ucheshi wake ulikuwa ni faraja katika kikundi”alisema Martha.

Naye mwandishi mwandamizi Felix Mwakyembe amesema tasnia imeondokewa na mwandishi mahiri ambaye alipenda kujifunza na kujiendeleza kielimu ambapo hadi umauti alikuwa akisoma Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji(TEKU)Mbeya.

Mmoja wa wanafunzi wa TEKU Shaban Nassoro Kisilwa amesema ndoto za mwenzao zimezimika ghafla kwani walitarajia kuhitimu naye mwaka huu.

Shughuli zote za msiba zinaratibiwa na Katibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Mbeya, Kenneth Mwakandyali ambapo amewataka waandishi kushirikiana katika kumsindikiza mwenzao katika safari yake ya mwisho.

Enzi za uhai wake marehemu amewahi kuhudumu kituo cha Radio cha Generation Fm na Baraka Fm akiwa masomoni.

Marehemu ameacha watoto watatu wawili wakiwa ni mapacha Bwana alitoa Bwana ametwaa jina la Bwana lihimidiwe.