May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mukoko awaangukia Yanga

Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

MCHEZAJI wa kikosi cha timu ya Yanga, Mukoko Tonombe amewaangukia mashabiki na viongozi wa benchi la ufundi kwa kitendo chake cha kumchezea rafu Nahodha wa Simba John Bocco katika mchezo wao wa Fainali wa Kombe la Shirikisho la Azam ‘Azam Sports Federation Cup’ uliochezwa jana jioni kwenye uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma.

Katika mchezo huo ambao Simba ilipata ushindi wa goli 1-0 lililofungwa dakika ya 80 na Taddeo Lwanga, Mukoko alipewa kadi nyekundu dakika ya 45 baada ya kumpiga kiwiko Bocco.

Kadi hiyo iliwagharimu Yanga ambao walilazimika kubadili mfumo wao na kucheza nyuma zaidi ili kulinda wasipoteze mchezo huo ambao walikuja kuruhusu goli hilo dakika za mwisho.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Mukoko ameandika kuwa “Nachukua fursa hii kuomba radhi mashabiki pamoja na viongozi na benchi la ufundi, kilichotokea katika mchezo wa fainali wa Yanga na Simba;

“Kwamba sikukusudia kupewa kadi nyekundu ambayo labda ndo ilikuwa sababu ya kupoteza mchezo huo, naipenda sana Yanga. Daima mbele nyuma mwiko,’.