July 21, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mradi wa maji wafikia asilimia 68

*Zaidi ya wananchi 12,000 kunufaika na mradi huo

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online- Mwanza 

WANANCHI zaidi ya 12,000 wa Kata ya Usagara wilayani Misungwi mkoani Mwanza, wanatarajia kunufaika na mradi wa uboreshaji wa mfumo wa usambazaji maji unaotekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza (MWAUWASA) kupitia ujenzi wa tenki la maji lenye uwezo wa lita milioni 1,linalojengwa katika Kata hiyo pamoja na ulazaji wa mabomba makuu ya kusafirisha maji.

Mradi huo ambao sasa umefikia asilimia 68, ni sehemu ya utekekalezaji wa mradi mkubwa uliwekwa jiwe la msingi Januari 23,2026 na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Mwigulu Nchemba,unahusisha ujenzi wa matenki matano ya maji yenye jumla ya ujazo wa lita milioni 31 yanayojengwa katika maeneo ya Buhongwa, Fumagila, Nyamazobe, Kisesa na Usagara.

Ofisa Maendeleo ya Jamii wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mwanza(MWAUWASA),Judith Mtui( mwenye nguo ya kijani),akizungumza katika kikao cha mamlaka hiyo na wananchi wa Mtaa wa Nyang’homango Kata ya Usagara wilayani Misungwi mkoani Mwanza, watakaonufaika na mradi wa uboreshaji wa mfumo wa usambazaji maji kupitia ujenzi wa tenki la maji la lita milioni 1, linalojengwa katika Kata hiyo.(Na Mpiga picha wetu)

Unaojumuisha ujenzi wa vituo viwili vya kusukuma maji katika maeneo ya Sahwa na Butimba pamoja na ulazaji wa mabomba makuu ya kusafirisha maji yenye urefu wa kilomita 40.5,ukiwa na thamani ya sh.bilioni 46.2.

Hayo yamebainishwa na Msimamizi wa Miradi wa MWAUWASA,Mhandisi Nuhu Said,katika kikao cha mamlaka hiyo na wananchi wanufaika wa Mtaa wa Nyang’homango Kata ya Usagara wilayani Misungwi kilichojadili kuhusu maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo.

Ambapo amesema,mradi huo kwa upande wa Usagara unahusisha ujenzi wa tenki la maji la lita milioni 1 litakalopokea maji kutoka tenki jipya linalojengwa eneo la Kagera-Buhongwa la lita milioni 10, sambamba na ulazaji wa mabomba makuu ya kusafirisha maji kwa urefu wa km10.5.

“Baada ya ujenzi wa matenki kukamilika kazi ya kuweka mtandao wa usambazaji maji itaanza rasmi,”amesema Mhandisi Said.

Muonekano wa tenki la maji lenye ujazo wa lita milioni 10 linalojengwa eneo la Kagera-Buhongwa

Akizungumza kwa niaba ya wananchi, Mwenyekiti wa Mtaa huo, Anthon Kalongo,amesema jitihada endelevu zinazofanywa na Serikali kupitia Wizara ya Maji na MWAUWASA za kuendelea kuwafikishia wananchi huduma hiyo muhimu katika maeneo mbalimbali ni hatua itakayo changia kuboresha maisha ya watu na kuchochea maendeleo.

Muonekano wa tenki la maji lenye ujazo wa lita milioni 1 linalojengwa eneo la Usagara