April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Miaka 60 ya Muungano Ilala yajivunia kuajiri walimu 150 kwa mapato ya ndani

Na Agnes Alcardo,Timesmajira Online,Dar

MKUU wa wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo,amesema kuelekea kilele cha miaka 60 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Aprili 26,2024,Halmashauri yake imefanikiwa kuajiri Walimu 150 wa michapuo ya sayansi kwa miakataba ya muda kutokana na mapato yake ya ndani.

Mpogolo, ameyasema hayo Aprili 16, 2024, katika Ukumbi wa Mikutano wa Jiji wa Arnatoglo, uliopo Jijini Dar es Salaam, kwenye mkutano uliohudhuriwa na Maafisa Elimu Kata, Wakuu wa Shule na walimu hao wa mikataba huku akitaja lengo la kutolewa kwa mikataba hiyo 150 tegemeo ni kuongeza ufaulu katika shule za sekondari zote wanapopangiwa walimu hao wa Mikataba.

Ambapo amewataka kuwa wazalendo na kufanya kazi Kwa uweledi na kuzingatia nguzo tano,ambazo ni Upendo kwa wanafunzi,kuishi vizuri na jamii kwa kujua mila na desturi zao, kufanya kazi kwa tija ili kukidhi aja ya mwajiri, kutimiza majukumu ya kazi za ualimu na maadili mema pamoja na kufanya kazi kwa bidii.

“Kuelekea kilele cha miaka 60 ya Muungano, Ilala tunayo mengi ya kujivunia katika kipindi chote hicho ikiwa pamoja na Halmashauri kupitia fedha zake za mapato imeweza kuajiri walimu wa michepuo wa sayansi 150 kwa mikataba ya muda.

“Hili ni jambo la kujivunia, hivyo ni vyema na nyie mkafanya kazi kwa weledi na kuzingatia nguzo tano katika utekelezaji wa majukumu yenu”, amesema Mpogolo.

Amewasihi kila mmoja hususani walimu hao walioaminiwa, kufanya kazi Kwa ufasaha, kwani mafanikio yaliyotaja katika halmashauri hiyo ni matokeo ya ukusanyaji mzuri wa mapato yake, huku akieleza kuwa, huo ni wito ambayo Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, amekuwa akisisitiza mara kwa mara katika mikutano na vikao vyake vya ndani.

Aidha ameeleza kuwa, Wilaya ya Ilala ina kila sababu ya kujivunia kwa yale mazuri na mafanikio waliyopata, huku akidai Wilaya hiyo kujiwekeza lengo la ukusanyaji wa mapato bilioni 89 na kusema kuwa mpaka sasa tayari imefanikiwa kukusanya zaidi ya bilioni 80, huku akieleza kuelekea kulifikia lengo la Rais Dkt. Samia la bilioni 120.

Amesema, mafanikio hayo pia ni pamoja na upande wa uboreshwaji wa miundombinu ya ujenzi wa madarasa na maabara, huku akieendelea kuwasisitizia walimu hao, kutumia vizuri haki na maonyo ya watoto na kukemea uwepo wa michango shuleni isiyo na tija inayoleta kero kwa wazazi na kusema kuwa, mwalimu yoyote anayefanya kazi Kwa mkataba atekayeenda kinyume atakua amejiondolea sifa ya kuendelea na ajira.

Hata hivyo, Mstahiki Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Omary Kumbilamoto, amemshukuru Mkuu huyo wa Wilaya kwa jitihada ambazo ameendelea kufanya katika Halmashauri hiyo, hususani katika upande wa elimu, huku akisema,kuwa wao kama Jiji wataendelea kuonesha ushirikiano na kufuata maelekezo yatayotolewa.