May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgogoro wa ardhi Nyandoto wakosa muafaka, wananchi wasisitiza maelekezo ya Waziri Mabula

Na Timothy Itembe,TimesMajira,Online, Mara.

BAADHI ya wawakilishi wa wananchi walikokuwa wameitwa ofisi ya halmashauri ya Mji wa Tarime kupokea maelekezo ya mgogoro wa Nyandoto wameshindwa kufikia muafaka kutokana na kile kilichodaiwa kuwa wanashinikizwa kununua viwanja badala ya kupimiwa walipie gharama za upimaji.

Wananchi hao wameshindwa kufikia muafaka huo hivi karibuni walipoitwa kwenye ofisi za halmashauri kwa ajili ya mgogoro huo kupatiwa ufumbuzi, lakini muafaka haukupatikana.

Mmoja wa wananchi hao, Alani Okelo amepongeze watu wa halmashuri ya Mji wa Tarime kwa kuwaita ili watatue mgogoro wa Nyandoto, lakini wanachosikia ni kile kile cha siku zote, kwani hakuna jipya.

Amesema wanaomba maelekezo ya Naibu Waziri Nyumba Maendeleo na Makazi, Angella Mabula aliyoyatoa mjini Musoma juu ya mgogoro huu yafuatwe, kwa sababu walikaa naye na akawasikiliza na alisema amegundua halmashauri walikwenda kupima maeneo yao bila kuwashirikisha wananchi.

“Sasa inakuwaje mrudie maelezo yenu yale yale ya kila siku, ambayo tunalalamikia kila siku tunaomba maelekezo aliyowapa Naibu waziri,” amesema Okelo.

Okelo aliongeza kuwa wameondolewa hadhi ya kuwa wamiliki ardhi yao, licha ya kuwa Naibu Waziri, Mabula aliwasikiliza na kugundua kuwa halmashauri ilipima viwanja kwenye maeneo yao bila kuwashirikisha.

Amesema wanataka warudishiwe maeneo yao na wapimiwe viwanja kwa kushirikishwa kwa kutumia wataalamu wa Serikali na walipie gharama za upimaji na kupewe muda wa kulipia na kwa atakaye shindwa kulipia atanyanganywa na halmashauri itaenda kumuuzia mwingine, lakini wanachokutana nacho sasa ni halmashauri kuwapimia ili walipie gharama za viwanja vilivyopimwa kama wengine walioomba, jambo ambalo hawakubaliani nalo, kwani wao ndiyo wamiliki wa maeneo hayo.

Naye Butebi Moya amelisema kuwa viongozi ndio mnaowayumbisha na kuanzisha mgogoro maeneo yao.

“Inakuwaje mnatuambie kuwa tulipie gharama za kununua viwanja vyetu kama watu wengine! Tunaomba tupimiwe tulipie gharama za upimaji viwanja sio kununua viwanja ambavyo ni maeneo yetu,” amesema.

Kwa upande wa Kaimu Mkurugenzi,Erasto Mbunga amewasihi wawakilishi hao kukubali maelekezo waliopatiwa na viongozi wao kutoka ngazi za juu yakiwemo ya Kamishina wa Ardhi Mkoa Mara, Mkuu wa Mkoa Mara na Naibu waziri nyumba na maendeleo ya makazi ya kuwataka watume maombi ili kupatiwa viwanja na walipie kwa muda mwafaka kama wengine walivyoomba.

Mwanasheria wa Halmashauri,Haruna Matata amesema tumewaita kwa ajili ya kuwapa maelekezo ya viongozi waliowaelekeza kukaa na nao kutatua mgogoro kufuatia maelekezo ya mkuu wa mkoa kupitia mkutano wa wananchi uliofanyika Agosti 13, mwaka huu pamoja na maelekezo ya Naibu Waziri, Mabula aliyoyatoa Agosti 8, 2021 mjini Musoma kuhusu mgogoro wa eneo lililopimwa viwanja Mtaa wa Nyagesese na kama hawatakubaliana na hayo, basi waende mahakamani.

“Tunafahamu wananchi 122 wanalalamika licha ya kuwa hawana uhalali wa maeneo hayo ,tunaomba waombe maombi ya kupewa viwanja kama wengine wanavyoomba na watapewa kipaumbele kwanza,” amesema Matata.