May 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mawaziri wa Fedha wasisitizwa mapambano dhidi ya ukatili

Na Penina Malundo

Mawaziri wa Fedha na Mawaziri wa Jinsia barani Afrika wametakiwa kuhakikisha suala la kupambana na ukatili wa kijinsia linawekwa kwenye Sera, mipango na bajeti za nchi ili litekelezwe kikamilifu.

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima ametoa wito huo Novemba 17, 2023 jijini Dar Es Salaam wakati akifunga mkutano wa siku tatu wa Mawaziri hao.

Amesema nchi zikiweka suala la ukatili wa kijinsia kwenye Sera, mipango na bajeti itasaidia kufikia usawa wa kijinsia kwa vitendo kama ilivyokusudiwa kwenye maazimio ya mikutano mbalimbali na kuweza kuyapima utekelezaji wake.

Waziri Dkt. Gwajima amesema masuala mengine ni kuwawezesha wanawake kiuchumi ili kuweka usawa na haki katika umiliki wa rasilimali, ubunifu na teknolojia, ushiriki wa wanawake katika masuala ya Amani na usalama ikiwemo kupata elimu kuhusu mabadiliko ya tabia nchi pamoja na suala la Afya kwa wanawake.

Ameongeza kwamba Serikali ya Tanzania imeshaanza kushirikiana na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhakikisha masuala ya jinsia yanajumuishwa katika mipango na bajeti na kukaguliwa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF AfRITAC East) Dkt. Xiangming Li, amesema washiriki wamehamasika na jinsi Tanzania inavyotekeleza suala la ushirikishwaji wa wanawake kupitia uongozi thabiti wa Dkt. Samia Suluhu Hassan