May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mashindano ya riadha ‘Mazingira Marathon’ kuanza kutimua vumbi Septemba 25

Na Bakari Lulela,TimesMajira Online, Dar

TAASISI ya Amon Mkonga Chief Promotions imeandaa mashindano ya riadha yajulikanayo kama “Mazingira Marathon” ikiwa lengo ni kuiunga mkono Serikali ya Awamu ya Sita katika kuhamasisha jamii kutunza mazingira.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi mtendaji wa taasisi hiyo Amon Mkonga amesema kwamba mashindano hayo yanatarajiwa kufanyika septemba 25 mwaka huu katika viwanja vya farasi ilivyoko jijini Dar es salaam.

Amesema kuwa mashindano hayo yatawashirikisha wanariadha kutoka ndani ya Tanzania na nchi za jirani ikiwemo nchi ya Kenya, ambao washiriki zaidi ya elfu tatu wanatarajiwa kuhamasisha upandaji miti ili kutunza uoto wa asili ambao unaonekana kupotea kila siku zinavyozidi kuendelea.

Mkurugenzi wa taasisi ya Amon Mkonga chief Promotion ya Dar es Salaam Amon konga (kushoto) akiwa na wadau wengine wa mashindano hayo akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusiana na mashindano ya riadha yajulikanayo kama ‘Mazingira Marathon ambayo yanatarajia kuanza kutimua vumbi Septemba 25, mwaka huu,.,

Amesema kwamba mashindano hayo ya riadha yameandaliwa kwa ushirikiano na wahisani mbalimbali ikiwemo kampuni ya Kinglion ,kampuni ya bia ya serengeti, pamoja na kampuni ya Cocola ambapo kwa pamoja wameamua kumuunga mkono rais Samia Suluhu Hassan wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye amekua mstari wa mbele kuihamasisha jamii katka utunzaji wa mazingira.

“Ndugu waandishi wa habari sisi kama taasisi tumeamua kutekeleza agizo la rais wetu mama Samia Suluhu Hassan kama mlivyomsikia amekuwa akitumia hotuba zake kuhamasisha jamii kutunza mazingira, tumeamua kuandaa mashindano haya ili kumuunga mkono,” amesema Amon.

Nakuongeza kuwa” kuhusu zawadi za washindi bado tunajaribu kuweka mambo sawa tukikutana katika mkutano ujao na nyinyi tutawatangazia watanzania wajue ni zawadi gani tutatoa kwa wanariadha watakaoshiriki, tunaomba jamii iendelee kutuunga mkono.

Kwa upande wake Mtendaji mkuu wa Kampuni ya Kinglion Ratnakar Waghi amesema kwamba taasisi ya Amon Mkonga Chief Promotions imeandaa jambo la muhimu katika maisha ya Watanzania kwani linalenga kulinda mazingira lakini pia kusaidia kuimarisha afya zao hususani katika kipindi hiki cha mlipuko wa virusi vya corona.

“Tumeamua kumuunga mkono , ni jambo zuri sana sisi kama kampuni ya Kinglion tunawajibika pia katika kutunza mazingira kwa hiyo mbio hizi zitasaidia sana kuendeleza kampeni hizi za kuhamasisha jamii kutunza mazingira” amesema

Mmoja wa washiriki wa mbio za riadha katika mashindano hayo Chacha Boy (27),kwamba nia yake nikupata ushindi wa nafasi ya kwanza lakini pia kuitangaza Tanzania kimataifa katika mbio za half Marathon zitakazofanyika nchi za Ulaya.