April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un yupo hoi kitandani baada ya kufanyiwa upasuaji mara kadhaa

Marekani yafuatilia afya ya Kim Jong Un

WASHINGTON, Serikali ya Marekani imedai inafuatilia taarifa za kiintelijensia zinazoelekeza kuwa, Kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un yupo hoi kitandani baada ya kufanyiwa upasuaji mara kadhaa.

Moja ya chanzo kutoka vyombo vya ulinzi na usalama vililieleza shirika la habari la CNN kuwa, Marekani imeendelea kufuatilia kwa karibu zaidi ripoti ya afya inayomuhusu Kim.

Kim hivi karibuni halishindwa kushiriki katika sherehe muhimu za kumbukizi ya kuzaliwa babu yake ambayo hufanyika kitaifa kila ifikapo Aprili 15,hali iliyozua taharuki nchini humo kuhusiana na afya yake.

Kabla ya sherehe hizo alikuwa ameonekana siku nne kabla akishiriki moja ya vikao vya Serikali.

Afisa mwingine wa Marekani aliieleza CNN kuwa, suala la afya ya Kim si rahisi kuweza kujulikana kwa sababu, ni vigumu kupata taarifa za kina juu yake kutoka nchini humo.

Naye Mshauri Mkuu wa Masuala ya Usalama wa Taifa nchini Marekani, Robert O’Brien alisema,Marekani zaidi juu ya ripoti za afya ya Kim.

“Tunazifuatilia ripoti hizi kwa karibu sana,”alisema O’Brien wakati wa mahojiano na Shirika la Habari la Fox News, na kuongeza kuwa, “Kama unavyojua, Korea Kaskazini ni jamii iliyofungamana kwa karibu zaidi”.

Awali, mmoja wa maafisa wa Jeshi la Ulinzi la Marekani alieleza kuwa, licha ya kufuatilia kwa karibu juu ya kudhoofika kwa afya ya Kim, lakini bado wanaendelea kuichukulia hali hiyo kwa tahadhari zaidi.

Kwa mujibu wa gazeti mtandao la Daily NK la nchini Korea Kusini,Kim anadaiwa kuugua kutokana na uvutaji sigara kupita kiasi, tatizo la moyo, uzito mkubwa na kufanya kazi kupitiliza.

Hata hivyo, Serikali ya Pyonyang imesema kiongozi wake Kim Jong Un hajalazwa kitandani na haumwi kama inavyodaiwa na Marekani na vyombo vingine duniani na muda wowote itatoa taarifa kamili.