May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mamia wamzika Baba wa Waziri Masauni

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Zanzibar

Wakazi wa Zanzibar na Vitongoji vyake wameungana na familia ya Marehemu Mzee Masauni Yussuf Masauni katika ibada ya maziko, Mzee Masauni alifariki majuzi katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kuzikwa katika Makaburi ya Mwanakwereke huku maziko hayo yakihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wa serikali na wastaafu huku yakiongozwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar,Hemed Suleiman Abdulla.

Awali Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,Dkt Hussein Ali Mwinyi alifika eneo la Migombani Wilaya ya Mjini Unguja nyumbani kwa Marehemu Mzee Masauni kuipa pole familia na kuwataka kuwa na subra baada ya kumpoteza mzazi wao huku akisifu utumishi uliotukuka wa marehemu katika kipindi chote alichohudumu katika nyadhifa mbalimbali za utumishi wa umma.

‘Natambua na kukumbuka nafasi na nyadhifa mbalimbali alizotumikia Mzee Masauni akiwa mtumishi wa umma huku mchango wako ukiiletea maendeleo nchi ya Zanzibar,natoa pole kwa nyie familia,ndugu,jamaa,marafiki na Watanzania kwa ujumla,tumuombe mungu ailaze roho ya marehemu mahala pema peponi’ alisema Rais Mwinyi

Akizungumza kwa niaba ya familia baada ya ibada ya maziko,Msemaji wa familia Abdallah Miraji Othman alimshukuru Rais wa Zanzibar,Dkt.Hussein Ali Mwinyi na viongozi mbalimbali akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Hemed Suleiman Abdula,Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati,Dkt.Dotto Biteko,Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,Dkt.Amani Abeid Karume na viongozi wengine kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiwemo mawaziri na Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama.

Katika utumishi wake wa umma marehemu Mzee Masauni alihudumu katika nafasi mbalimbali huku nafasi ya mwisho aliyoshika ni Kamishna wa Idara ya Uhamiaji Zanzibar ambapo alistaafu rasmi mwaka 1985.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Alhajj Hemed Suleiman Abdulla akiweka mchanga katika kaburi wakati wa mazishi ya Mzee Masauni Yussuf Masauni ambae ni Baba Mzazi wa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi,Mhandisi Hamad Masauni swala ya maiti imefanyika msikiti wa Kilimani na kuzikwa kwenye Makaburi ya Mwanakwerekwe Visiwani Zanzibar.Picha na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi