April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Madiwani Bukoba Vijijini wampongeza Rais Samia

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira,Online,Dar

MADIWANI wa Halmashauri ya Bukoba Vijijini (CCM), wamepongeza Serikali kwa kazi kubwa ya ujenzi wa miundombinu na kushauri kasi hiyo iendeleee kwenye miradi yote ya kimkakati.

Pia madiwani hao wameipongeza Serikali ya awamu ya tano na ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa namna inavyotekeleza miradi hiyo kwa vitendo

Wameyasema hayo jana jijini Dar es Salaam walipotembelea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Terminal III, Daraja la Mfugale, Daraja la Nyerere Kigamboni, Reli ya Kisasa (SGR) na Daraja la Tanzanite

Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), Dk. Jasson Rweikiza akiwaelekeza jambo madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini na kamati ya siasa ya wilaya hiyo walipotembelea shule ya St Anne Marie Academy Mbezi Kimara kwa Msuguri jijini Dar es Salaam Madiwani hao wako kwenye ziara ya kutembelea miradi mbalimbali kwenye ziara ya mafunzo kwa uratibu wa mbunge huyo.

Madiwani hao walikuwa jijini Dar es Salaam kwa ziara ya mafunzo kwa mwaliko wa Mbunge wa Jimbo hilo, Dkt. Jasson Rweikiza, ambapo pia walitembelea miradi mbalimbali mkoani Dodoma kabla ya kuja Dar es Salaam

Kwenye ziara hiyo wameambatana na Sekretarieti ya CCM Wilaya Wilaya ya Bukoba Vijijini na Kamati ya Siasa ya Wilaya hiyo.

Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Diwani wa Kata ya Kanyangereko, Joasi Rweikiza amesema wamejionea wenyewe utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati kama Serikali ilivyoahidi.

Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), Dkt. Jasson Rweikiza mbele mwenye miwani akiwaongoza madiwani 31 wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini na wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Wilaya hiyo kwenye uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Terminal III, walipoenda kutembelea uwanja huo.

“Tulikuwa tunasikia tu lakini kwa ziara hii tumejionea wenyewe na tunakwenda kuwaambia wananchi kwamba Serikali ya CCM inatekeleza Ilani ya chama kwa vitendo waendelee kuiunga mkono,” amesema

Alisema madiwani wenzake wamefurahishwa mno na kuona uwanja wa ndege mpya kwa namna ulivyojengwa kwa kwa viwango vya kimataifa

Amesema ujenzi wa barabara ya njia nane kutoka Mbezi kuelekea Kibaha Mkoa wa Pwani imeondoa tatizo la foleni ambalo lilisumbua kwa muda mrefu.

Amesema watu walikuwa wakitumia muda mrefu kutoka jijini Dar es Salaam kufika Kibaha lakini ujenzi wa barabara hizo umepunguza muda na kwa sasa dakika 20 tu zinatosha kufika Kibaha

Diwani wa Kata ya Buterankunzi, Gospel Mashongole, alisema wamejifunza kwa vitendo mambo mengi ambayo awali walikuwa wakiyasikia tu kwenye vyombo vya habari.

Madiwani 31 wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini na wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Wilaya hiyo wakiwa kwenye picha ya pamoja na mbunge wao kwenye uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Terminal III, walipoenda kutembelea uwanja huo.

“Mfano ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR kutoka Dar mpaka Mwanza tulikuwa hatujawahi kuona lakini leo tumeona wenyewe sasa tunawaambia watu waliokuwa wanabeza kwamba mambo yanafanyika kwa vitendo,” amesema

Amemshukuru Mbunge wa Bukoba Vijijini, (CCM), Dk. Jasson Rweikiza kwa ziara hiyo ya mafunzo ambayo alisema imewafumbua macho madiwani hao kwani awali hawakuwahi kujionea wenyewe utekelezaji wa miradi hiyo

Naye Dkt. Rweikiza amesema dhumuni la ziara hiyo ni kujifunza na walianzia Dodoma ambapo walijifunza mambo mbalimbali yanayofanywa na Bunge.

Amesema madiwani hao wamejionea wenyewe utekelezaji mkubwa wa miradi mbalimbali na wameahidi kwenda kuwaeleza wananchi kwamba serikali waliyoiweka madarakani inatekeleza ahadi zake kwa vitendo

Mbunge wa Bukoba Vijijini (CCM), Dkt. Jasson Rweikiza mbele mwenye miwani akiwaongoza madiwani 31 wa Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba Vijijini na wajumbe wa Kamati ya Siasa ya Wilaya hiyo kwenye uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Terminal III, walipoenda kutembelea uwanja huo.

“Miezi mitatu iliyopita kuna Sh bilioni 1.5 zilitolewa jimboni kwangu kwaajili ya kukarabati barabara kuna miradi mingi ya maji ambayo inatekelezwa jimboni kwa hiyo serikali inachapa kazi na wananchi waendelee kuiamini,” amesema

“Sasa hawa madiwani walipenda waje Dar es Salaam na mikoa mingine kuangalia utekelezaji kwa vitendo na kwa kweli wamefurahi na kumpongeza Rais Samia na CCM kwa kutekeleza Ilani ya chama kwa vitendo,”amesema Rweikiza