May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

LSF yajadili na kutathmini utekelezaji wa upatikanaji haki nchini

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online, Dodoma

SHIRIKA lisilo la kiserikali la Legal Services Facility (LSF), limezindua mkutano wa siku tatu unaoshirikisha washiriki zaidi ya 400 kutoka kwenye mashirika yanayotoa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria takriban 200 yanayopokea ruzuku kwa ajili ya utekelezaji wa programu ya upatikanaji wa haki nchini.

Mkutano huu unalenga kujadili na kutathimini utekelezaji wa upataikanaji wa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria nchini, mafanikio, changamoto, fursa na mipango mikakati kwa ajili ya utekelezaji wa programu ya upatikanaji wa haki nchini katika kipindi cha mwaka mmoja ujao 2022/2023.

Akiongea jana kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa LSF, Meneja Programu kutoka LSF,Wakili Deogratias Bwire aliwapongeza wasaidizi wa kisheria na mashirika ya wasaidizi wa kisheria kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa kuiwezesha jamii hususani wanawake na watoto wa kike kupata haki zao.

“Tunajivunia mafanikio tuliyoyapata mwaka jana, wasaidizi wa kisheria wameweza kuwafikia wananchi takriban milioni 7 katika elimu ya kisheria na kupokea migogoro 88,000 ambapo tariban migogoro 65,000 imeweza kutatutuLIwa na wasadizi wa kisheria,” alisema Meneja Programu LSF.

Wakili Bwire aliongeza kwa kusema kuwa, mkutano huu wa siku tatu utawezesha wadau wa LSF ambao ni mashirika nufaika kutoa mrejesho wa utekelezaji wa shughuli za msaada wa kisheria, kubadilishana uzoefu na kujifunza mbinu mbalimbali kwa ajili ya kujijenga na kujiimarisha kwenye masuala yote yanayohusu huduma za msaada wa kisheria.

“Natoa wito kwa washiriki wa mkutano kuzitumia siku za mkutano kikamilifu. Ni matuamini yangu kikao hiki kitajadili na kutoka na mapendekezo, mikakati ya utekelezaji ili kuongeza tija na kuboresha ubora wa utoaji wa huduma za msaada wa kisheria ili kupata matokeo chanya katika jamii.”

“Hii ni muhimu kwetu kama wasimamizi wa ruzuku tunazozitoa kutoka kwa wadau wetu wakubwa ambao ni Shirika la Kimataifa la Maendeleo la nchini Denmark (DANIDA). Ili kujenga jamii iliyowezeshwa kisheria,” alisisitiza Wakili Bwire.

Akiongea kwa niaba ya Msajili wa Huduma za Msaada wa Kisheria Wizara ya Katiba na Sheria, Wakili wa Serikali, Wakili Agnes Mkawe aliwashukuru na kupongeza uongozi wa LSF kwa kuandaa warsha hii muhimu kwa mustakabali na ustawi wa wadau wa sekta ya msaada wa kisheria na huduma, ambao kwa namna moja au nyingine inaendelea kujenga ushirikiano na uhusiano mzuri baina ya LSF na Serikali.

“Tunaomba ushirikiano huu uendelee zaidi na zaidi katika kuhakikisha huduma ya msaada wa kisheria unaotolewa unakuwa wenye tija na manufaa kwa umma wa Watanzania. Sisi kama Serikali pia tunawashukuru wadau wa maendeleo kama Shirika la Kimataifa kutoka Denmark (DANIDA) kwa kuwawezesha LSF ili waweze kutekeleza programu yao, ambayo imekuwa ni muhimu kwa wananchi wengi,” amesema Wakili Mkawe.

Aidha alisema, Wizara ya Katiba na Sheria imeendelea kutambua mchango mkubwa unaotolewa na wadau wote wa huduma ya msaada wa kisheria katika utoaji wa huduma hiyo kwa wananchi.

Sekta hii ndogo ya utoaji huduma ya msaada wa kisheria imeonekana kuwa yenye umuhimu mkubwa kutokana na juhudi zinazofanywa na Serikali pamoja na wadau wote wa msaada wa kisheria ambao baadhi yao ni ninyi mliopo hapa leo.

Aidha, Wakiili Mkawe ameongeza kwa kusema

”pamoja na kazi nzuri inayofanywa na watoa huduma ya msaada wa kisheria nchini Wizara bado inaona changamoto kubwa bado ipo kwa wasaidizi wa kisheria na mashirika yao kujisajili kwenye mfumo wa kieletroniki, takwimu ya usajili kwa njia ya mfumo inaonyesha ni mashirika yapatayo 220 na Wasaidizi wa Kisheria wapatao 1047 ndio waliosajiliwa.”

“Hii inatia doa sana sana kwa sekta hii ndogo ya msaada wa kisheria ambayo ni mtakumbuka kwa kuwa awali ilidaiwa kuwa ada ya usajili wa Wasaidizi wa Kisheria ilikuwa kikwazo kwa usajili. Serikali, kwa usikivu wake, na kwa kutambua hali halisi ya mazingira mnayofanyia kazi, iliondoa takwa hili ambalo kimsingi ilikuwa katika mamlaka ya Waziri.”

Wakili Mkawe alieleza zaidi kuwa pamoja na hatua hiyo ya serikali, ongezeko la usajili tangu lilipotolewa tamko na Mhe Waziri wa Katiba na Sheria hadi leo ni Wasaidizi wa Kisheria wachache sana ukilinganisha na wale ambao Msajili mwenyewe amewapa vyeti vya mafunzo.

“Huu sio tu ukiukwaji wa sheria na kuyataka mashirika ya msaada wa kisheria na watoa huduma wa msaada wakisheria kumaliza usajili wa mashirika yao mara moja,” alieleza Muwakilishi huyo wa Msajili wa Huduma za Msaada wa Kisheria.

Kwa upande wa washiriki wa mkutano wameipongeza LSF kwa kuendelea kutoa ruzuku ya utekelezaji wa mradi wa upatikanajia haki na kuwezesha huduma za msaada kuwa endelevu.

Vilevile, waliomba changamoto mbalimbali wanazokumbana nazo wakati wa uteekelezaji wa mradi zikiwemo ukubwa wa nchi katika baadhi ya maeneo yanayowafanya washindwe kuwafikia wananchi, vitendea kazi zinazoweza kuendana na kukua kwa matumizi ya teknologia, mafunzo ya kiprogram kifedha, na utawala bora ziweze kututatuliwa Mkutano huo wa siku tatu umeshirikisha watendaji wa idara mbalimbali za mashirika nufaika ya LSF ikiwemo programu, fedha, wakuu wa taasisi/mashirika hayo pamoja na wawakilishi wa bodi kutoka katika mikoa yote Tanzania bara na Zanzibar.

Muwakilishi wa Msajili wa Huduma za Msaada wa Kisheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria nchini, Wakili Agness Mkawe akizungumza na watoa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau uliondaliwa na LSF pamoja na wadau wake nchini nzima kwa ajili ya kutathmini utekelezaji za programu ya upatikanaji wa haki nchini inayotekelezwa na LSF.
Washiriki wa mkutano wakifuatilia mkutano wa wadau uliondaliwa na LSF pamoja na wadau wake nchini nzima kwa ajili ya kutathmini utekelezaji za programu ya upatikanaji wa haki nchini inayotekelezwa na LSF.
Meneja Programu wa Legal Services Facility (LSF), Wakili Deogratias Bwire akizungumza na watoa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau uliondaliwa na LSF pamoja na wadau wake nchini nzima kwa ajili ya kutathmini utekelezaji za programu ya upatikanaji wa haki nchini inayotekelezwa na LSF.
Muwakilishi wa Msajili wa Huduma za Msaada wa Kisheria kutoka Wizara ya Katiba na Sheria nchini, Wakili Agness Mkawe akiwa kwenye picha ya pamoja na watoa huduma za msaada wa kisheria na wasaidizi wa kisheria wakati wa ufunguzi wa mkutano wa wadau uliondaliwa na LSF pamoja na wadau wake nchini nzima kwa ajili ya kutathmini utekelezaji za programu ya upatikanaji wa haki nchini inayotekelezwa na LSF.