May 14, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kupitia mradi wa Vijana na Mkwanja,vijana wameweza kuanzisha biashara 17

Na Judith Ferdinand,TimesMajira Online, Mwanza

Imeelezwa kuwa jumla ya biashara 17,zimeanzishwa na vijana kutoka Kata 6 zilizopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela,kupitia mradi wa Vijana na Mkwanja.

Ambapo mradi wa Vijana na Mkwanja,ulianza mwaka 2019 mpaka sasa upo katika awamu ya tatu ya utekelezaji na unatekelezwa na shirika la Mtandao wa Watoto na Vijana Mwanza(MYCN) chini ya ufadhili wa The Foundation For Civil Society (FCS) huku lengo ni kuhakikisha vijana wanajikwamua kiuchumi kwa kufanya biashara zao na kumiliki mali.

Akizungumza katika siku ya jukwaa la maendeleo ya kiuchumi kwa vijana kupitia mradi huo ambao uliwakutanisha viongozi mbalimbali wa halmashauri ikiwemo Madiwani pamoja na Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza na vijana ambao ni wanufaika wa mradi,lililofanyika jijini Mwanza.

Ofisa Mradi wa Vijana na Mkwanja kutoka MYCN James James,ameeleza kuwa kupitia mradi huo vijana waliokuwa nao sasa wanaongezeka na mafanikio yanaonekana.

“Sasa mwaka 2022 tupo awamu ya tatu ya utekelezaji wa mradi huu na tunajionea mafanikio ambayo yapo kwa vijana ambapo zaidi ya biashara 17 zimeanzishwa kitu ambacho akikuwepo na zinafanywa na vijana tofauti tofauti,wameweza kutafuta fursa ambazo zinawazunguka,wameweza kuzalisha na kuingia katika soko la ushindani kulingana na kile wanachozalisha hiyo yote ikiwa ni katika kuhakikisha lile lengo la wao kujikwamua kiuchumi linakamilika,”amesema James.

James ameeleza kuwa,kitu kikubwa kwenye mradi ilikuwa ni kuhakikisha vijana wanaweza kunyanyuka kiuchumi na kuweza kuanzia biashara zao na kumiliki mali ambapo wanufaika wa moja kwa moja wa mradi huo ni vijana 151 kutoka vikundi sita katika Kata sita za Kitangiri,Nyamanoro, Buswelu, Ilemela, Nyasaka na Shibula wilayani Ilemela.

Pia akizungumzia lengo la kuwa na jukwaa hilo la siku moja amesema ni kuwakutanisha vijana hao na viongozi ambao wanamchango chanya katika maendeleo,ili wajionee nini kinafanywa na vijana na viongozi wachangie namna gani ya kuendelea kuwasaidia vijana kufikia malengo yao.

Ofisa Ufuatiliaji na Tathimini wa MYCN Rahel Zakayo, amesema vijana hao wamefanikiwa kuanzisha biashara ikiwemo utengenezaji wa viatu vya ngozi,maua,viungo vya chakula,sabuni za maji,usindikaji wa mvinyo,peanut butter ( karanga za kusagwa),unga lishe,ufugaji wa kuku,uuzaji wa parachichi,sabuni za vipande pamoja na ushonaji.

“Siku ya leo tumekuja hapa kwa pamoja vijana na viongozi wetu pamoja na wadau kutoka mashirika mbalimbali kwa lengo kubwa la kukutana hapa ni sisi vijana kujadili kwa pamoja mambo ambayo tunayafanya sisi, shughuli zetu za uzalishaji lakini viongozi na wadau wetu kuona na kuongeza tija kwa kile ambacho vijana wanaweza kuzalisha tuwe na maendeleo endelevu na sisi katika mradi wetu tuweze kufika lengo letu la kuinua vijana kiuchumi,”amesema Rahel.

Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza Isaac Ndassa, amesema vijana wanachangamoto nyingi kuanzia katika hali halisi ya wao kujitambua na mara nyingi wanakuwa na mawazo ya kupewa kitu wafanye kitu na maisha yao yanategemea watakuwa vipi.

Ndassa amesema,katika kuwainua vijana wameisha anza kupitia mashirika mbalimbali kwa kuwapeleka SIDO vijana ili waweze kupata mafunzo na ujuzi kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali na kuhakikisha shughuli zao zinasimamiwa na kufuatiliwa kwa karibu sana na waratibu wa Serikali.

“Mfano kama vijana wameamua kuanza shughuli ya bajaji basi mapato yao yanapaswa kusimamia vizuri ili yaweze kufanya shughuli nyingine au kuongeza bajaji au kuzalisha shughuli ambazo zitawafanya wajitegemee, kuhakikisha kuwa miradi ambayo imezoeleka vijana wasijifunge wafanye miradi mingine mikubwa ambayo inafaida ili wasimame na waweze kuwa matajiri,” amesema Ndassa.

Baadhi ya wanufaika wa mradi huo akiwemo Christian Chacha, amesema ameishukuru MYCN pamoja na wadau wengine na serikali kwa mafanikio walio yapata kikundi kuongezeka kutoka watatu hadi sita.

“Changamoto yetu kwa sasa ni mtaji kwani lengo letu ni tuwe na viwanda viwili vya kuchakata mvinyo(wine) na karanga(peanut butter) lakini katika hili pia tuweze kutoa ajira kwa vijana na tulionao ajira kwa vijana ni chache na tukiweza kuwa na viwanda hivyo tutakidhi soko la ajira kwa vijana wenzetu,”amesema Chacha.

Ofisa Mradi wa Vijana na Mkwanja kutoka MYCN James James, akizungumza katika siku ya jukwaa la maendeleo ya kiuchumi kwa vijana kupitia mradi huo ambao uliwakutanisha viongozi mbalimbali wa halmashauri ikiwemo Madiwani pamoja na Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza na vijana ambao ni wanufaika wa mradi,lililofanyika jijini Mwanza. (Picha na Judith Ferdinand)
Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza Isaac Ndassa,akizungumza katika siku ya jukwaa la maendeleo ya kiuchumi kwa vijana kupitia mradi huo ambao uliwakutanisha viongozi mbalimbali wa halmashauri ikiwemo Madiwani pamoja na Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza na vijana ambao ni wanufaika wa mradi,lililofanyika jijini Mwanza. (Picha na Judith Ferdinand)
Mmoja wa wanufaika wa mradi wa Vijana na Mkwanja Christian Chacha,akizungumza katika siku ya jukwaa la maendeleo ya kiuchumi kwa vijana kupitia mradi huo ambao uliwakutanisha viongozi mbalimbali wa halmashauri ikiwemo Madiwani pamoja na Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza na vijana ambao ni wanufaika wa mradi,lililofanyika jijini Mwanza. (Picha na Judith Ferdinand)
Baadhi ya wanufaika wa mradi wa Vijana na Mkwanja wakiwa na bidhaa zao wanazozalisha waliohudhuria siku ya jukwaa la maendeleo ya kiuchumi kwa vijana kupitia mradi huo ambao uliwakutanisha viongozi mbalimbali wa halmashauri ikiwemo Madiwani pamoja na Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza na vijana ambao ni wanufaika wa mradi,lililofanyika jijini Mwanza. (Picha na Judith Ferdinand)