May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kuhuisha mikakati inasaidia kuendeleza halmashauri

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia masuala ya TAMISEMI Bw. Sospeter Mtwale amewataka Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa sehemu ya Mipango na Uratibu kufanya uhuishaji wa Mipango Mikakati ya Mikoa na Serikali za Mitaa ili isaidie Serikali kuendelea kupanga mipango ya maendeleo kwa wananchi.

Mtwale ameyaeleza hayo leo Disemba 18, 2023 Mkoani Morogoro wakati akifungua mafunzo ya Kuhuisha Mpango Mkakati (Strategic Plan -SP) wa Taasisi kwa Makatibu Tawala Wasaidizi wa Mikoa sehemu ya Mipango na Uratibu katika Mikoa na utekelezaji wa majukumu ya kila siku.

Mtwale amesema uzoefu umeonesha uwepo wa matumizi ya Mipango Mkakati ambayo haihuishwi kwa wakati na baadhi ya Mikoa na Halmashauri hivyo, kusabisha changamoto mbalimbali katika Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya kila mwaka kukosa mwelekeo na mkanganyiko ndani ya Mkoa na Halmashauri.

“Bila Mpango Mkakati uliohuishwa watumishi na wadau ndani ya Mkoa au Halmashauri wanaweza kuandaa mipango yenye mwelekeo tofauti hivyo, kutokuwa na manufaa yanayoonekana” amesema Mtwale

Aidha, amesema kuwa na mipango mkakati iliyopitwa na wakati na takwimu zilizopitwa na wakati haiwezi kuendana na malengo ya sasa ya Mkoa au Halmashauri kwani italeta hali ya kutofautiana kwa vipaumbele na kurudisha nyuma juhudi za kuwaletea wananchi maendeleo.

Aidha, Mtwale amewasisitiza maafisa hao kufanya kazi kwa ufanisi hali wakitumia Mpango Mkakati uliohuishwa ambao unaoweza kujipima kila wakati kuona kama malengo yaliyowekwa yamefikiwa.

Kwa upande wa Mkurugenzi Msaidizi Sehemu ya Uratibu wa Shughuli za Serikali Ofisi ya Rais -TAMISEMI Bw. Johnson Nyingi amesema, mafunzo hayo ya siku mbili yatakwenda sambamba na kujifunza Muundo Mpya wa Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Mikoa, na Halmashauri mwaka 2022, Changamoto za Muundo Mpya wa Ofisi za Wakuu wa Mikoa na MSM, Muundo, Mchakato/Hatua na Vigezo katika Uandaaji wa Mipango Mikakati ya Taasisi na Uhuishaji wa Mipango Mikakati ya Mikoa kwa kuzingatia Muundo Mpya wa Mikoa.

Naye Katibu Tawala Msaidizi, Mipango na Uratibu Mkoa wa Dar es Salaam, Chillah Mosses ameishukuru Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa kuendelea kutoa mafunzo akielezea kuwa mafunzo husaidia kuongeza ujuzi na kuboresha utendaji kazi katika majukumu ya kazi na kuahidi kuyafanyia kazi yale yote waliyoelekezwa kwa manufaa ya wananchi.