May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Masasi yajipanga kuanza kujitegemea yenyewe

Na Mwandishi Wetu,Timesmajira,Online

KUELEKEA  miaka 100 ya Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Masasi itakayotimizwa mwaka 2026, waumini wa dayosisi hiyo wametakiwa kuanza kujitegemea badala ya kutegemea misaada kutoka mataifa ya nje.

Hayo yamasemwa na Askofu wa Dayosisi hiyo, Dkt. James Almasi katika ibada ya kutabaruku kanisa kuu la Mariam Mbarikiwa na Bartholomayo Mtume wilayani Masasi hapa amesema dayosisi yao  ni miongoni mwa dayosisi 28 kongwe kuzaliwa ndani ya kanisa la Anglikana Tanzania.

Amesema dayosisi hiyo ilianzishwa mwaka 1926  jambo ambalo linaifanya wilaya ya Masasi kutengeneza historia kubwa katika nyanja za utume na uinjilisti pamoja na huduma za jamii.  

Amesema Dayosisi hiyo ilizaliwa ikiwa na watumishi wazalendo wachache  huku Askofu na watumishi wengine wengi wakiwa ni raia wa kigeni hivyo uendeshwaji wa taasisi hizo ulitegemea  sadaka za wakristo na uwezo wa wazungu.

“Hali hiyo imeendelea hadi hivi sasa jambo ambalo lilifanya na limeendelea kudumaza maono yetu kuona kwamba hatuwezi kufanya sisi wenyewe pasipo misaada,”amesema na kuongeza

“Hali ya kukosa maono makubwa ya kusaidia dayosisi imefanya taasisi za kanisa hilo yaani za afya na elimu nziendeshwe kwa kusuasua ikiwemo ujenzi wa nyumba za kuabudia, usomeshwaji wa wachungaji na watumishi wa ofisi kuu na za taasisi kwa sehemu na asilimia zaidi ya 95 umetegemea wafadhili na vyombo vya usafiri katika ngazi zote pia,”Amesema

 Amesema wamekusudia kubadilisha hali ya dayosisi yao kwa wahudumu na waumini wote kuondoa dhana ya kutegemea msaada na kuanza kujitoa kwa dhati ili kusaidia kazi ya Mungu.

Amesema Dayosisi imedhamiria kupanda makanisa kadhaa na uanzishwaji wa parish mpya, ujenzi wa majengo mengine ikiwemo shule za wavulana Rondo na wasichana Namasakata, vile vile wanahitaji kusomesha wahudumu, kwa gharama za kanisa lenyewe  ambapo

Askofu Dkt. James amesema hayo hayawezekani bila waumini wa kanisa hilo kwenda pamoja ili kumtendea Mungu haki kwa kushindwa kufanya mambo makubwa yenye kuinua utukufu wa Mungu.

Alimtaka kila muumini kwa nafasi yake atambue na kuchukua hatua ya maumivu lakini yenye ukombozi mbele kwani jitihada za kupanda makanisa na uanzishwaji wa parish mpya ni budi iendane na kusomesha wahudumu kwa gharama za Dayosisi yenyewe ili kuendana na kauli mbiu ya ‘Inawezekana tuanze sasa’.