May 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Jukwaa la uwezeshaji wanawake Dodoma watembelea hifadhi ya Taifa Ruaha

Na Doreen Aloyce ,Timesmajira Online, Iringa

Katika juhudi za kuendelea kumuunga Mkono Rais Samia Suluhu Hassani za kuutangaza Utalii hapa Nchini Mamlaka ya Hifadhi ya Taifa (Tanapa) Mkoa wa Dodoma kwa kushirikiana jukwaa la uwezeshaji wanawake kiuchumi Dodoma wametembelea Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kwa ajili ya kutalii pamoja na kujifunza tabia za wanyama jambo ambalo litasaidia kuwa na manufaa kwa jamii.

Akizungumza na Gazeti hili jana Kamishna Msaidizi mwandamizi wa hifadhi Ofsi ya Dodoma ,Dkt Noelia Myonga amesema kuwa utalii huo umehusisha watu wa rika zote wakiwemo Jukwaa la uwezeshaji wanawake Dodoma,wawekezaji,wajasiliamali na wasanii lengo likiwa ni kuhamasisha utalii kwa makundi yote.

Amesema kuwa kutokana na uwepo wa makao makuu Jijini Dodoma kuna haja ya kuhamasisha utalii kila mahali na makundi mbalimbali ya kitanzania badala ya kusubiri wageni kutoka nje ya nchi.

“Tumeweza kuandaa safari na watu wameweza kuwa na mwitikio mkubwa kuonyesha elimu inaendelea kuenea kwenye jamii na tutambue kuwa tunapotembelea hifadhi tunajifunza mambo mengi ikiwemo tabia za wanyama ,wadudu na mimea hivyo kila mtanzania aone umuhimu”amesema Dkt. Noelia Myonga.

Hata hivyo ametoa wito kwa jamii inayozunguka Mto Ruaha uliopo ndani ya hifadhi kutunza mto huo badala ya kutumia kwa ajili ya shughuli za kilimo jambo ambalo upelekea changamoto ya kukosekana kwa umeme unaotumiwa kwenye hifadhi .

Nae Afisa Mkuu wa Uhifadhi ya Taifa ya Ruaha Marckyfarreny Rwezaula ambaye ni Kaimu mkuu wa Hifadhi amesema hifadhi hiyo inaweza kupokea watalii miatano kwa siku licha ya changamoto mbalimbali walizonazo ikiwemo ya ubovu wa Barabara ambayo tayari Serikali imeweka mkakati wa kuijenga kiwango cha lami kuanzia Iringa mpaka Hifadhini.

“Lakini pia tuna mpango wa kujenga maeneo ya malazi kwa ajili ya wageni pamoja na kufungua mageti ambayo yatasaidia watalii wa ndani kutoka mikoa ya Mbeya na Njombe kuwa rahisi kuingia hifadhini balada ya kuzunguka ikiwa ni pamoja na kujenga viwanja vya ndege. ” amesema Dkt. Rwezaula.

Nae Afisa Mwandamizi wa Uhifadhi Amina Salum, ambaye ni msimamizi wa kitengo cha Utalii Ruaha amesema katika hifadhi hiyo kuna vivutio mbalimbali ya wanyama na ndege pamoja shughuli mbalimbali zikiwemo utalii wa magari, wa ndege, kuvua samaki, kutembea kwa magari , na kutembea kwa miguu .

“Hapo mbeleni tutakuwa na watalii wengi wa ndani tofauti na hapo awali na ni kutokana na Rais wetu Samia Suluhu Hassani kutangaza utalii hivyo tuendelee kumuunga mkono” amesema Afsa mwandamizi Amina.

Mwenyekiti jukwaa la uwezeshaji wanawake Wilaya ya Dodoma Marry Barnabasi amesema kuwa ili kuendelea kuunga juhudi za Rais Samia wanawake wakiamua utalii utaongezeka kwa kiasi kikubwa hapa nchini.

Amesema Zoezi hilo la utalii ni mwendelezo wa kila mwezi ambao umeandaliwa na jukwaa la uwezeshaji wanawake Dodoma kutangaza vivutio mbalimbali hapa nchini.