May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Jaji Mkuu: WCF inagusa ustawi wa wananchi

NA K-VIS BLOG/KHALFAN SAID, KIGOMA

JAJI Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Profesa Ibrahim Hamisi Juma, amesema Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema lengo la vyombo vyote vya dola ni ustawi wa wananchi.

Mhe. Jaji Mkuu, ameyasema hayo mjini Kigoma Aprili 19, 2024, wakati akifungua  Kikao Kazi kati ya Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Mahakama ya Tanzania na Watendaji wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) mjini Kigoma lengo kuu likiwa ni kujenga uelewa wa Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi.

“WCF ni Mfuko unaogusa ustawi wa wananchi, kwasababu unaweza kuwa unamtegemea mama, kaka, bahati mbaya akapata ajali akafariki, hapa ustawi wa familia unaweza kutoweka, kama hakuna Mfuko unaoweza kubeba hilo jukumu, kwa hivyo huu Mfuko ni muhimu mno mno.” Amebainisha Mhe. Profesa Juma.

Aidha Mhe. Profesa Juma amehimiza umakini na uadilifu katika utekelezaji wa sheria hiyo ya Fidia kwa Wafanyakazi.

“Ukosefu wa umakini, udanganyifu vyote vimechangia kuua mifuko ambayo ilikuwa na malengo mazuri sana. Tusipokuwa waangalifu, mfuko huu wa WCF vile vile unaweza kukumbana na tatizo hili. Tukielewa vizuri mantiki ya kuanzishwa mfuko huu tutaufanya uwe endelevu na himilivu,” amesema.

Aidha Mhe. Jaji Mkuu ameipongeza WCF kwa kupiga hatua kubwa katika matumizi ya TEHAMA katika utekelezaji wa majukumu yake na kukumbusha umuhimu wa mifumo ya taasisi za umma kusomana ili kurahisisha utoaji wa huduma.

“Ifike mahala mfanyakazi anapowasilisha madai yake WCF, mfumo mzima uwe unaelewa kwamba mfanyakazi fulani amepata ajali kazini au amefariki. Mifumo ya serikali ikiweza kutambuana pia itasaidia sana kuziba mianya ya udanganyifu.” Alisisitiza.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Emmanuel Humba, amemuhakikishia Mhe. Jaji Mkuu kwamba Mfuko unaendeshwa kwa ufanisi mkubwa na umepata mafanikio makubwa katika kutekeleza malengo yake.

“Malipo ya fidia kwa Wafanyakazi yameongeza kutoka TZS 3.88 bilioni Kwa mwaka 2016/2017 hadi kufikia TZS 23.58 bilioni kwa mwaka 2022/2023. Hili ni ongezeko kubwa la malipo ya fidia kulinganisha na kiasi cha TZS 250 milioni zilizokuwa zikilipwa na Waajiri kwa mwaka kabla ya kuanza Mfuko.” Amefafanua Bw. Humba.

Aidha, michango ya Waajiri iliyokusanywa imeongezeka kutoka TZS 68.40 bilioni Kwa mwaka 2015/2016 hadi kufikia TZS 86. 48 bilioni kwa mwaka 2022/2023, amesema Bw. Humba.

“Faida inayotokana na uwekezaji ya fedha zilizobaki baada ya kulipa mafao imeongezeka kutoka TZS 1.60 bilioni Kwa mwaka 2015/2016 hadi kufikia TZS 102.43 bilioni kwa mwaka 2022/2023, lakini pia   thamani ya Mfuko imeongezeka kutoka TZS 65.68 bilioni Kwa mwaka 2015/2016 hadi kufikia TZS 602.78 bilioni kwa mwaka 2022/2023.” Amefafanua.

Kuhusu ustahamilivu wa Mfuko katika kutekeleza majukumu yake, Mwenyekiti huyo wa Bodi amesema kuwa tathmnini ya uhai na uendelevu wa Mfuko iliofanywa na Shirika la Kazi Duniani (ILO) inaonesha kwamba Mfuko unauhimilivu (Sustainability) kwa kipindi cha miaka 30 kuanzia mwaka wa tathmini 2022/2023.

Akizungumzia kuhusu nia ya kikao kazi hicho, Bw. Humba alibainisha kuwa pamoja na kwamba jukumu la kulipa fidia limekasimiwa kwenye Mfuko, Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi imeweka utaratibu na vyombo vya kushughulikia madai ya wanufaika pale wanapokuwa hawajaridhika na fidia iliyolipwa au maamuzi ya Mfuko yanayokinzana na matarajio yao.

Akifafanua zaisdi alisema, Sheria inamtambua Waziri Mwenye dhamana ya masuala ya kazi kuwa ni Mamlaka ya kwanza ya rufaa dhidi ya uamuzi wa Mfuko na Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi kuwa Mamlaka ya mwisho ya rufaa.

“Kutokana na hitaji hili muhimu la kisheria, Bodi ya Wadhamini ya WCF, Menejimenti ya Mfuko pamoja na Watendaji wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi waliona kuna hitaji la kufanya vikao kazi kwa lengo la kubadilisha uzoefu, kujenga uelewa wa pamoja na kubainisha maeneo ya sheria yanayohitaji maboresho kwa lengo la kuongeza ufanisi katika kutekeleza Sheria hiyo.” Alisema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma ameeleza kuwa ushirikiano baina ya Mfuko na Mahakama ni muhimu kwa vile kuna maeneo mengi ambayo Mfuko unakutana na Mahakama katika utekelezaji wa majukumu yake.

“Sisi kama WCF shughuli zetu hazikamiliki bila ya uwepo wa shughuli za Mahakama. Kwa mfano katika kushughulikia masuala yanayohusu mirathi, Mfuko hutegemea maamuzi ya Mahakama.” Alisema Dkt. Mduma.

Awali, akizungumza kabla ya kumkaribisha Jaji Mkuu kufungua Kikao Kazi hicho, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambia alisema kuwa kumekuwa na vikao kazi vitano ambavyo vimefanyika baina ya Mahakama, WCF na Watendaji wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) huko Bagamoyo, Mwanza, Arusha, Songea na Kigoma.

Alibainisha kuwa jumla ya Viongozi na watumishi 290 wameshiriki katika Vikao Kazi hivyo, wakiwemo Majaji 70, Naibu Wasajili 33, Watendaji 11, Wadau 48, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi 32 na zaidi ya watumishi wa Mahakama 96.

JAJI Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Profesa Ibrahim Hamisi Juma, akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi baina ya WCF, Mahakama na CMA mjini Kigoma Aprili 19, 2024
JAJI Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Profesa Ibrahim Hamisi Juma, akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao kazi baina ya WCF, Mahakama na CMA mjini Kigoma Aprili 19, 2024
Kikao kikiendelea
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw. Emmanuel Humba, akieleza mafanikio mbalimbali ambayo Mfuko umeyapata tangu kuanzishwa kwake
Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Dkt. John Mduma, akieleza jinsi Mfuko unavyotekeleza kwa vitendo Tunu (Core value) ya Ushirikiano na taasisi zingine ikiwemo Mahakama.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Kazi, Mhe. Dkt. Yose Mlyambia, akkeleza matokeo ya vikao kazi hivyo katika kuboresha Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi.
Baadhi ya washiriki wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa kikao kazi hicho.
Baadhi ya washiriki wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa kikao kazi hicho.
Mkurugenzi wa Huduma za Tathmini WCF, Dkt. Abdulsalaam Omar, yaya aliwasilisha mada iliyoelezea mambo mbalimbali ikiwemo jinsi tathmini za ulemavu zinavyofanyika ikiwa ni seehemu ya mchakato wa kulipa fidia.
Mkurugenzi wa Uendeshaji WCF, Bw, Anselim Peter, yeye aliyoa mada kuhusu uendeshaji wa shughuli za Mfuko, ikiwa ni pamoja na utaratibu wa kuwasilisha madai.
Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Sheria, WCF, Bw. Abrahamu Siyovelwa, akitoa mada kuhusu Sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi.
Kamishna wa Kazi, Bi. Suzan Mkangwa akiwa ni miongoni mwa viongozi walioshiriki katika kikao hicho.