May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ilala yatakiwa kutumia vizuri mapato ya ndani

Na Heri Shaban, Timesmajira Online,Ilala

Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo, ameitaka Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kufanya kazi vizuri kwa kutumia fedha za mapato ya ndani .

Mkuu wa Wilaya ya Ilala Edward Mpogolo, amesema hayo wakati wa kuzindua magari ya wagonjwa (Ambulance) saba ziliofanyiwa ukarabati kwa fedha za mapato ya ndani ambayo yamesambazwa vituo vya afya kwa ajili ya kutoa huduma .

“Nawaomba watendaji wa Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam mfanye kazi kwa weledi na ushirikiano huku mkitumia fedha za mapato ya ndani vizuri katika utekelezaji wa majukumu yenu,” amesema Mpogolo.

Mpogolo amesema Ilala sasa hivi ni faraja Idara ya Afya ya Halmashauri ya Jiji imefanya vizuri hivyo watumishi wa afya wa halmashauri hiyo wafanye kazi kwa ushirikiano katika kuisaidia Serikali ili malengo waliojiwekea yaweze kutimia

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Zaituni Hamza, amesema mara baada kufika Ilala alipewa maelekezo ya kazi huku akitakiwa kujipanga katika kutekeleza majukumu na kutoa huduma bora kwa jamii ndani ya wilaya Ilala.

Hamza amesema Idara ya Afya imekusanya fedha za kutosha ikiwa ni juhudi zake katika usimamizi mkubwa kwa ushirikiano na watendaji wake na watumishi .

Amesema mikakati ya idara ya afya Halmashauri ya Jiji hilo inatarajia kufungua chuo cha afya ndani ya wilaya Ilala.

Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Jomary Mrisho Satura amesema magari yote saba ya wagonjwa yametengezwa kwa wakati mmoja ambayo yamegharimu milioni 24 sasa hivi yanasambazwa vituo vya afya kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi.

Satura amewataka watumishi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam katika sekta nyingine kujifunza kwa sekta ya afya mikakati yao ili na wao waweze kufikia malengo Ilala iweze kusonga mbele katika idara zote.

Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM)Wilaya ya Ilala Said Sidde, alimpongeza Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo kwa utendaji bora wa kazi na ubunifu ambapo amewataka wakuu wa idara wa Halmashauri ya Jiji hilo kuiga mfano huo na ubunifu ulitumika huku akiwataka madereva waliopewa dhamana kusimamia magari hayo na kuyatunza .