May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ilala inawawezesha wanawake na vijana kunufaika kiuchumi

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online, Dar es Salaam.

WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Doroth Gwajima, amesema asilimia kubwa ya mapato yanayoongezeka nchini kwa kiasi kikubwa, yanatokana na mapato ya wajasiriamali wanawake na vijana.

Gwajima ameyasema hayo leo Jijini Dar es Salaam, wakati akifungua maonesho maalumu ya wajasiriamali wanawake wa Mkoa wa Dar es Salaam, yaliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Ilala, yanayofanyika katika Viwanja vya Mnazi Mmoja na kutarajiwa kumalizika Septemba 13 mwaka huu.

“Napenda kuwapongeza wajariamali wote waliojitokeza kwa wingi kushiriki katika maonesho haya kwani hii ni fursa kubwa mno..lakini pia naomba mtambue kuwa asilimia kubwa ya mapato yanavyoongezeka nchini yanatokana na mapato ya wajasiriamali wanawake na vijana”, alisema Gwajima.

Pia amesema kuwa, mikopo mbalimbali inayotolewa na Serikali kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali wanawake na vijana, imechangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi wa nchi.

“Lakini pia mikopo mbalimbali inayotolewa na Serikali kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali wanawake na vijana, imechangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi wa nchi yetu, hili ni jambo zuri mno”, alisema.

Gwajima pia amewataka wajasiriamali hao wanawake, kuacha kuchukua mikopo ya mitaani huku akitolea mfano “Mikopo ya Kausha damu”, Kwa madai kuwa mikopo hiyo haitawaletea maendeleo bali itawashusha kiuchumi.

Aidha, Gwajima ameipongeza Benki ya CRDB Nchini, kupitia Taasisi yake ya ‘CRDB Foundation’ kuja na mpango wa kuwawezesha Vijana na Wanawake unaojulikana kama iMbeju, ambayo imeonekana kuwa msaada mkubwa kwa watanzani hasa wajasiriamali kunufaika kiuchumi.

Nae Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, ambaye pia alimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila, amesema mapato yaliyokusanywa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilala ni zaidi ya Bil.27, kiasi ambacho kimetokana na mikopo ya Serikali ya Asilimia 10 iliyokuwa ikitolewa na Kwa wanawake, vijana, na makundi maalumu ya watu wenye ulemavu.

“Kutokana na maonesho haya kuwa na tija, hivyo napenda kusema kuwa maonesho haya yatakuwa endelevu katika Wilaya yetu ya Ilala, lengo likiwa ni kuwawezesha wanawake na vijana kunufaika kiuchumi na kuondokana na umaskini..

Aidha Mpogolo amesema kuwa, maonesho hayo yatakuwa endelevu katika Wilaya ya Ilala, yakiwa na lengo la kuwawezesha wanawake na vijana kunufaika kiuchumi na kuondokana na umaskini lakini pia, mapato yaliyokusanywa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilala ni zaidi ya Bil.27, kiasi ambacho kimetokana na mikopo ya Serikali ya Asilimia 10 iliyokuwa ikitolewa na Kwa wanawake, vijana, na makundi maalumu ya watu wenye ulemavu.

Zaidi ya wajasiriamali wanawake Elfu Moja, kutoka Wilaya zote tano za mkoa wa Dar es Salaam, wameshiriki katika maonesho hayo yaliyoandaliwa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Ilala kwa kudhaminiwa na Benki ya CRDB.