April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Huawei kuwekeza Dola mil. 150 ukuzaji vipaji vya dijiti

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira,Online,Dar

KAMPUNI ya Huawei imepanga kuwekeza dola za Marekani milioni 150 katika kukuza vipaji vya dijiti katika kipindi cha miaka mitano ijayo, mpango ambao unatarajiwa kufaidisha vijana wengine milioni 3.

“Tunatangaza muendelezo wa mpango wa mbegu za kizazi kijacho cha Huawei “Huawei’s Seeds for the Future Program 2.0”.

Kama sehemu ya ahadi yetu ya kuendelea kukuza vipaji, tutawekeza dola milioni 150 katika mpango huu kwa kipindi cha miaka mitano ijayo na kusaidia wanafunzi wa vyuo vikuu na vijana kuboresha ujuzi wao wa dijiti. Programu hii inatarajiwa kufaidisha watu wengine milioni 3,” alisema Mwenyekiti wa Huawei Liang Hua.

Mwaka 2008, Huawei ilianza kupanua programu zake za kukuza vipaji kupitia ufadhili wa masomo, mashindano ya teknolojia na mafunzo ya ustadi wa dijiti, ikiwa imewekeza zaidi ya dola milioni 150 za kimarekani katika programu hizo, huku ikinufaisha zaidi ya watu milioni 1.54 kutoka nchi zaidi ya 150 ulimwenguni.

Mpango huu unakusudia kukuza vipaji vichanga kutoka kote ulimwenguni, kuwapa mafunzo kutoka kwa wataalam wa ICT juu ya teknolojia ya kisasa ili kuwasaidia kukuza ujuzi na fikira zinazohitajika kuwa na ushindani katika mazingira ya kazi ya siku zijazo.

Huawei ilianzisha programu hii barani Afrika mwaka 2014. Katika miaka iliyopita, programu hiyo imewanufaisha karibu wanafunzi 2,000 kutoka nchi Zaidi ya 25 za Afrika. Mpango huo na juhudi za Huawei katika ukuzaji wa vipaji za ICT vimetambuliwa na Serikali nyingi za Afrika.

Kutoka kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Katibu Mkuu, Dkt. Leonard Akwilapo, alisifia mpango wa “Seed for the Future” na umuhimu wake katika kuwezesha ujuzi wa kuajiriwa.

“Mpango huu unadumisha ushirikiano kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Huawei Tanzania katika kukuza mahusiano endelevu ya rasilimali watu katika ICT. Programu hii inafanya kazi kama daraja ambalo linaziba pengo kati ya mafunzo ya kinadharia na mahitaji ya vitendo katika soko la ajira,” alisema

Yang Chen, Makamu Rais wa Huawei Kanda ya Kusini mwa Afrika, alisema Huawei imejitolea kwa maendeleo ya rasilimali watu Afrika.

“Afrika ina idadi kubwa ya vijana, vijana hawa ndio rasilimali kubwa ya bara hili ambayo itaimarisha uchumi katika siku zijazo. Huawei inashirikiana na serikali za Kiafrika, taasisi za elimu na tasnia ili kuwapa viongozi wa siku zijazo maarifa ya kisasa katika kiwango cha juu kabisa ulimwenguni huvyo kuwapa fursa ya kutumia maarifa hayo kuleta maendeleo barani.”