April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Hakimu, Mzazi mwenzake kufikishwa mahakamani

Na David John, Timesmajira Online

HAKIMU wa Mahakama ya Mwanzo Kilimatinde , Bahati Ilikunda na Mzazi mwenzake Haji Bwegege wapo mbioni kufikishwa mahakama Wilaya ya Manyoni na Taasisis ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Singida kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa kinyume na kifungu cha Sheria namba 15 ,cha Kuzuia na Kupambana na Rushwa namba moja ya mwaka 2007.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Arusha, Adili Elinipenda imesema, Ofisi yake ilipokea taarifa kutoka kwa mwananchi mmoja (jina lake limehifadhiwa) kuwa Hakimu Ilikunda wa Mahakama ya Mwanzo ya Kilimatinde Wilayani Manyoni aliomba rushwa ya Sh. 350,000 ili atoe upendeleo kwa mtoa taarifa katika shauri la madai namba 03 ya mwaka 2020.

“Tulipata taarifa Juni 28,2020 huko Wilayani Manyoni Mkoani Singida katika maeneo ya Kituo cha mabasi yaendayo Dodoma hivyo Ofisi yetu ilimkamata Haji Bwegege ambaye ni mzazi mwenzake Bahati baada ya kupokea rushwa ya kiasi cha Sh. 170,000 ikiwa ni sehemu ya Sh. 350,000 aliyoomba,” amesema.

Elinipenda amesema, kwenye taarifa hiyo kwamba uchunguzi wa Takukuru Mkoa humo umejiridhisha kuwa Bwegege na Bahati wana uhusiano wa kifamilia kwani wana mtoto waliyemzaa pamoja.

“Kutokana na uchunguzi wetu tumeona kuna jambo linaloashiria uwezekano wa Hakimu Bahati kumtuma Bwegege katika kupokea rushwa anazoziomba,” amesema na kuongeza

“Hata hivyo Ofisi yake inatoa shukrani za dhati kwa Idara ya Mahakama mkoani hapo kwa jinsi wanavyotoa ushirikiano kwenye mapambano dhidi ya rushwa kuanzia Mahakama ya Mwanzo hadi Mahakama ya Mkoa,” amesema Elinipenda.