May 14, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dkt.Angeline; viongozi tatueni migogoro ya ardhi

Judith Ferdinand,TimesMajira Online,Mwanza

Viongozi mbalimbali wenye dhamana kuanzia ngazi ya Mtaa mpaka Mkoa,wametakiwa kutatua migogoro ya ardhi ambayo imekuwa changamoto nchini.

Hayo yamezungumzwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt.Angeline Mabula,wakati wa kikao kazi cha viongozi wanaosimamia sekta ardhi kwa ngazi zote kuanzia wilaya , mitaa, kata na mkoa wa Mwanza,kilichofanyika Machi 9, mwaka huu jijini hapa.

Dkt.Angeline ameeleza kuwa katika Mkoa wa Mwanza kumekuwa na tatizo kubwa la kudhulumu ardhi kwa wazee na wajane. Huku utaratibu wa utoaji vibali vya ukarabati wa majengo umekuwa unakiukwa sana.

”Suala la utatuzi wa mgogoro wa ardhi sio suala la Wizara eti kusema kuna mawaziri nane, nitashangaa eneo lina mamlaka lakini mtu anasubiria Waziri, Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa wilaya, shughulikieni migogoro ya ardhi katika maeneo yenu,”ameeleza Dkt.Angeline.

Ili kuondokana na migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikitokea kati ya wananchi na wawekezaji,amezitaka halamshauri zote nchini kutenga maeneo ya uwekezaji na kuyalinda kwaajili ya kupokea wawekezaji.

“Wengi hawatambui kuwa sekta ya ardhi ni mtaji ukitumika vizuri inaweza kulisaidia taifa au mtu mmoja mmoja, kikao hiki tumepeana mambo matatu,usimamizi wa mpango kabambe wa Jiji la Mwanza na utekelezaji wake, programu ya urasimishaji makazi na kuzuia ujenzi holela,”ameeleza Dkt.Angeline.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Adam Malima ameeleza kuwa kamati za ardhi zinashida hivyo ametumia fursa hiyo kumuomba Waziri huyo kushugulika na Wilaya ya Nyamagana kisha Wilaya ya Ilemela.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt.Angeline Mabula, akizungumza katika kikao kazi cha viongozi wanaosimamia sekta ardhi kwa ngazi zote kuanzia wilaya , mitaa, kata na mkoa wa Mwanza,kilichofanyika Machi 9, mwaka huu jijini hapa.
Baadhi vya wadau waliohudhuria kikao kazi cha Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt.Angeline Mabula,na viongozi wanaosimamia sekta ardhi kwa ngazi zote kuanzia wilaya , mitaa, kata na mkoa wa Mwanza,kilichofanyika Machi 9, mwaka huu jijini hapa.