May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Diwani Mgitu amshukuru Rais Samia ujenzi kituo cha afya Kinyerezi

Na Heri Shaaban, TimesMajira Online

Diwani wa Kata ya Kinyerezi Leah Mgitu ,amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan, kwa kuwekeza sekta ya afya kata ya Kinyerezi kuwajengea mradi wa kisasa wa kituo cha afya.

Diwani Leah Mgitu, alisema hayo katika ziara yake ya Halmashauri Kuu ya kata na Kamati ya Siasa kuangalia utekelezaji wa Ilani katika miradi mkubwa wa Rais ambao umejengwa kata ya Kinyerezi uliozinduliwa na Mwenge wa UHURU Mei 8 mwaka huu.

“Natumia fursa hii kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji wa Ilani ya chama cha Mapinduzi (CCM )pamoja na ushirikiano mzuri uliopo wa Mbunge wangu wa jimbo la Segerea Bonnah Ladslaus Kamoli Kinyerezi sasa tunajivunia kituo cha afya cha Kisasa chenye vifaa vya kisasa vyote vipo pamoja na jengo la upasuaji ,Jengo la huduma la mama na Mtoto “alisema Leah.

Diwani Leah Mgitu alisema katika kata ya Kinyerezi anaishukuru Serikali ya Dkt.Samia na Mbunge Bonnah kwa kuwekeza miradi mikubwa ya maendeleo ambapo kila mwaka inapata fursa ya kuzinduliwa na Mwenge wa UHURU ikiwemo kituo cha Daladala cha kisasa.

Alipongeza uongozi wa Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam ukiongozwa na Meya wa Halmashauri ya jiji hilo Omary Kumbilamoto, Mkurugenzi wa jiji Jamary Mrisho Satura na Mganga Mkuu wa Halmashauri kwa utendaji bora wa kazi zao mpaka kuakikisha Kinyerezi maendeleo yanakuwa mwaka hadi mwaka .

Alitumia fursa hiyo kumuomba mganga mkuu wa Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam Zaituni Hamza katika kituo hicho cha afya Kinyerezi zijengwe hodi za Kisasa baadae Kinyerezi ikiwa Wilaya kituo hicho cha afya kipandishwe hadhi na kuwa Hospitali ya Wilaya Kinyerezi.

KATIKA hatua nyingine ameiomba Serikali ijenge zahanati kwa ajili ya wananchi wa KIBAGA ili iweze kuwahudumia wananchi wa eneo hilo ambao wanapata tabu huduma za afya zipo mbali na makazi yao kutokana na Jografia ya Kinyerezi na idadi ya wananchi kila siku wanaongezeka.

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya jiji hilo Dkt. Zaituni Hamza alisema kituo hicho cha afya ambacho kimezinduliwa na Mwenge wa UHURU ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ambapo kituo hicho chaAfya Kinyerezi jengo la OPD linavifaa vyote vya kisasa ikiwemo Otosaund
.


Dkt Zahtuni alisema katika kituo cha afya Kinyerezi ndio kituo cha kwanza cha afya Halmashauri ambacho kina uwezo wa kuangalia Tezi Dume,na maswala ya uzazi kwa wanawake pia kuna mashine bingwa na madaktari wa kisasa.

“Katika kipindi cha miaka Mitatu cha uongozi wa Dkt.Samia Halmashauri yetu ya jiji imeweza kupokea Ambulance sita mpya za wagonjwa ,mitambo ya sikoseli ya watoto ambapo dhumuni la Serikali kuondoa vifo vya watoto wachanga na Rais ameweza kutoa ajira mara mbili kwa watumishi sekta ya Afya “alisema Dkt Zaituni.