August 15, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Diwani aunga juhudi  ujenzi wa barabara

Na Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza

DIWANI wa Kata ya Nyamanoro wilayani Ilemela mkoani Mwanza,Abdulrahman Kange ameendelea kuunga mkono juhudi za wananchi wa Mtaa wa Nyamanoro Mashariki za kujenga barabara ya Sinza-Mjimwema kwa kiwango cha zege yenye urefu wa mita 500 kwa kutoa mifuko 10 ya saruji pamoja na kushiriki ujenzi wa barabara  hiyo unaoendelea.

Akizungumza  Agosti 15,2026 mara baada ya kukabidhi mifuko hiyo kwa Mwenyekiti wa Mtaa wa Nyamanoro Mashariki Missa Budundu,Kange amewapongeza wananchi wa mtaa huo kwa kujitolea kurekebisha na kujenga  barabara hiyo  kwa kuchangia mfuko mmoja  mmoja wa saruji kwa kila kaya.

Diwani wa Kata ya Nyamanoro wilayani Ilemela mkoani Mwanza,Abdulrahman Kange(wa pili kushoto),akikabidhi mfuko wa saruji Mwenyekiti wa Mtaa wa Nyamanoro Mashariki Missa Budundu(wa kwanza kulia)

“Kwa ushirikiano huo kati ya wananchi na viongozi,naamini muda si mrefu barabara hii itafika mwisho ili iweze kupitika vizuri na kusaidia vijana wetu,wanawake wanauza samaki  na watu mbalimbali hasa wenye ulemavu waweze kupitia vyema.Hivyo leo nimetoka mifuko10,huu ni mwanzo nitaendelea kuwashika mkono  ili kuhakikisha barabara yetu inakamilika,”amesema Kange.

Kange amesema, barabara hiyo hadi sasa inahitaji mifuko ya saruji 480 pamoja na mahitaji mengine ikiwemo mchanga na kokoto,hivyo ametoa wito kwa wadau na wananchi  kuendelea kuchangia ili barabara hiyo iweze kupitika huku ujenzi ukiwa  umefikia asilimia 45,hivyo matarajio yao kupitia michango ya wananchi na wadau ifikapo Desemba 2026,wanatarajia kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo.

Pia amesema,barabara hiyo inaunganisha kata hiyo na  kata jirani,na ni kiungo ambacho siyo tu kinasaidia wakazi wa Nyamanoro pekee pia wakazi wa mitaa na kata jirani  pamoja na kusaidia watu kufanya shughuli zao za maendeleo na kujipatia kipato.

Hivyo ametoa wito kwa viongozi wa Serikali za Mitaa na Halmshauri  kuunga mkono jitihada ambazo wananchi wa mtaa huo wamezionesha ili kuhakikisha ujenzi wa barabara hiyo inakamilika na kutoa huduma kwa jamii.

“Sisi wananchi wa Kata ya Nyamanoro tumeanza lakini tunahitaji Serikali itushike mkono kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa barabara hii,”amesema Kange.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Nyamanoro Mashariki Missa Budundu amesema,mtaa huo umepokea mifuko 15 ya saruji kutoka kwa Diwani huyo kwa ajili ya ujenzi wa barabara ambapo awali alitoa mifuko mitano na leo mifuko 10.

Amesema,ujenzi wa barabara hiyo ulianza mwaka 2024 mara baada ya kuingia madarakani kwa nafasi ya Unyekiti,na mpaka sasa wameisha jenga urefu wa mita 100 kati ya mita 500 kwa nguvu za wananchi na wadau.Hivyo amewasisitiza wananchi wa mtaa huo kutekeleza walichokubaliana kwa kila mmoja kuchangia ujenzi kwa kila kaya kutoa mfuko mmoja wa saruji 

“Bado mita 400 kukamilisha ujenzi wa barabara hii,na kila mita 25 tunatumia mifuko 30 ya saruji,hivyo bado tunahitaji mifuko 480 ya saruji,mchanga na kokoto,kwani barabara hii ni kiungo muhimu katika mitaa ya Nyamanoro na Kata jirani,”amesema Budundu.

Mmoja wa wananchi wa Mtaa wa Nyamanoro Mashariki Haruna Hamad amesema,ubovu wa barabara hiyo inawapa changamoto waendasha bodaboda na bajaji hasa kufikisha abiria,hivyo  ikikamilika itarahisisha usafiri kwa wananchi huku Anastasia David amesema,barabara hiyo ni  changamoto hasa kwa  wajawazito pindi wanapotaka kwenda hospitali  kujifungua.

Kwa upande wake Mjumbe wa Serikali ya Mtaa wa Nyamanoro Mashariki Kezia Manyama amesema,kutokana na ubovu wa barabara hiyo umesababisha watu kujifungua njiani hivyo wanaposhirikiana wanatoa kitu kizuri.

“Ombi langu Serikali ituangalie kwa machi mawili,maana mtaa huu kuna wengine hawana kitu hivyo  kufanya ujenzi unakuwa changamoto na wakati mwingine kushindwa kukamilisha,”amesema Manyama.

Baadhi ya wananchi wataa wa Nyamanoro Mashariki Kata ya Nyamanoro wilayani Ilemela wakichanganya zege Kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Sinza-Mjimwema