April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Dhahabu Kilo 9 yakamatwa Jijini Mbeya ikitoroshwa

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online. Dar

JESHI la Polisi Mkoani Mbeya, linawashikilia wafanyabiashara wa madini 10 kwa tuhuma za utoroshaji wa madini Kilogramu 9.8 yenye thamani zaidi ya shilingi bilioni 1

Akitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa habari,Waziri wa Madini, Anthony Mavunde, amesema wafanyabiashara hao walikamatwa siku ya Jumamosi Majira ya saa 10:27 Alfajiri Katika mtaa wa Ilomba Jijini Mbeya, kwenye nyumba waliyokuwa wamepanga wakiwa na vipande 344 ya dhahabu iliyochomwa.

Dhahabu hiyo yenye uzito wa Kilogramu 9.8 pamoja na vifaa mbalimbali kama vile Precious Metal analayzer (XRF) aina ya Niton DXL thermoscientific, mitungi ya gesi, jiko na vyungu kwa ajili ya kuchomea dhahabu, Kipimo cha maji cha kupimia dhahabu, mizani kadhaa pamoja na kemikali aina ya borax.

WAZIRI Mavunde ameupongeza uongozi wa Mkoa wa Mbeya na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na Kikosi Kazi cha Wizara ya Madini kufanikisha ukamataji wa watuhumiwa hao.

Pia, Waziri Mavunde ametoa rai kwa wafanyabiashara wote wa madini, kuhakikisha wanazingatia sheria na kanuni za kufanya biashara ya madini nchini na wote watakaobainika kutorosha madini watachukuliwa hatua za kisheria pamoja na kufutiwa Leseni zao.

Aidha, Waziri Mavunde ameagiza kusimamishwa kwa Leseni za biashara ya Madini za watuhumiwa nchi nzima wakati taratibu za upepelezi zikiendelea kabla ya kufikishwa Mahakamani.

Akizungumza katika zoezi hilo, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya wa Chunya, Mbaraka Batenga, amewataka viongozi wote wa mitaa na vijiji, kuwatambua watu katika maeneo yao kwa kuwasajili katika daftari la wakazi na kuwataka wamiliki wa nyumba za kupanga kuhakikisha wanawafahamu vyema wapangishaji wao na shughuli zao.