May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

DC Mtanda awahakikishia ulinzi waandishi wa Afrika

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online, Arusha

MKuu wa Wilaya ya Arusha Said Mtanda amewakikishia usalama waandishi wa habari waliohudhuria maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya habari Duniani ambayo kwa Kanda ya Afrika yanayofanyika Jijini Arusha.

Ameyazungumza hayo leo katika maadhimisho yanayofanyika mkoani Arusha ambayo kilele chake ni kesho amesema kuwa viongozi wa mkoa huo wamejipanga vyema katika kuimarisha ulinzi.

“Tunatambua waandishi wengi wa habari wametoka sehemu mbalimbali duniani, naomba niwaondoe hofu kuwa Mkoa upo salama na tulivu, kama mlivyokuja salama, mtaondoka salama pia” amesema Mkuu wa wilaya.

Kwa upande mwingine, Mtanda amesema ujio wa ugeni huo ni neema kwa wananchi na Mkoa wa ujumla kwani umesaidia kuongeza kipato Cha mwananchi mmoja mmoja na Serikali kupitia huduma mbalimbali wanazopata na kwamba Serikali itahakikisha huduma hizo ni bora na za viwango vya kimataifa.Kwa mara ya kwanza maadhimisho hayo kwa Kanda ya Afrika yanafanyika nchini Tanzania katika Mkoa wa Arusha.

Maadhimisho hayo yalianza jana ambapo mada mbalimbali zimejadiliwa ikiwemo ukuaji wa teknolojia unavyoathiri tasnia ya habari huku kauli mbiu ya mwaka huu ya kimataifa ikisema Uandishi wa habari na changamoto za kidigitali.

Mei 3 kila mwaka dunia huadhimisha Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani ambapo Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye kilele cha maadhimisho hayo ya Kanda ya Afrika yanayofanyika kesho Jijini Arusha.