May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkuu wa Wilaya ya Ilala Gw'ilabuzu Ludigija (kushoto) akipokelewa na Katibu wa Umoja wa Wanawake Kata ya Buyuni Aziati Juma katika ofisi ya Kata katika ziara endelevu ya mkuu wa Wilaya kutatua kero za Wananchi

DC Ilala azishukia kampuni feki za upimaji

Na Heri Shaaban TimesMajira Online

MKUU wa Wilaya ya Ilala, Ng’wilabuzu Ludigija ametoa agizo kwa Afisa Ardhi Manispaa ya Ilala kuzihakiki upya kampuni za urasimishaji ardhi zilizopo katika Manispaa hiyo na kuzichukulia hatua kampuni zote watakazobaini ni feki.

Ludigija ametoa agizo katika Kata ya Buyuni Jimbo la Ukonga leo alipokuwa kwenye ziara yake endelevu Wilayani huyo yenye lengo la kutatua kero mbalimbali za Wananchi.

Amesema, kampuni zote za urasimishaji ardhi zilizochukua tenda ndani ya wilayani Ilala kama hawajamaliza kazi na mkataba umekwisha warudishe fedha za wananchi na Wizara wawafute hazifai.

“Kuna kampuni za urasimisha zinafanya utapeli nimepitia taarifa moja ya kampuni iliyochukua tenda Kata ya Buyuni toka mwaka 2019 mpaka sasa mkataba umekwisha kazi bado hajamaliza na kuleta kero kwa wananchi wamepeleka michoro Wizarani wamerudishwa naomba warudishe pesa kwa wananchi, ” amesema Ludigija.

Amesema kuwa, kampuni hiyo ilipewa mkataba wa miezi nane wawe wamemaliza kazi waliopewa kwani wananchi wakipata hati zao watakuwa uraisi kukopesheka na kuchukua mikopo mikubwa .

Pia amemtaka Afisa Ardhi Manispaa ya Ilala kuzifanyia uhakiki upya kampuni zote za urasimishaji zilizopewa tenda kuangalia mikataba yao kama kazi walipewa wamemaliza wasitumie ujanja ujanja na kama wameshindwa kazi hizo zitafanywa na wataalam wa Manispaa ya Ilala.

Kwa upande wake, Meneja DAWASA Mkoa wa Ukonga, Mponjoli Damsoni amesema, kuna mradi mkubwa wa maji wa Kisarawe Mkoa wa Pwani ambao mara baada kukamilika utasambaza maji katika kata za Majohe, Chanika, Buyuni, Pugu na mpaka Kivule dhumuni kumaliza changamoto ya maji kwa wakazi wa maeneo ya Jimbo la Ukonga.