April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza ACP. Muliro Jumanne

Dada wa kazi ashikiliwa kwa mauaji ya mtoto

Na Daudi Magesa TimesMajira Online, Mwanza

MTUMISHI wa kazi za ndani Ashura Suka (15) anashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza kwa tuhuma za mauaji ya mtoto mdogo wa mwajiri wake .

Mtoto huyo mwenye umri wa miezi 11 anadaiwa kuuawa Agosti 23, mwaka huu, saa 4:30 asubuhi, nyumbani kwa wazazi wake, Kata ya Iloganzala, Manispaa ya Ilemela.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Jumanne Muliro amethibitisha kutokea kwa tukio hilo la mauaji na kueleza kuwa wanamshikilia Ashura ambaye ni mkazi wa Nyamanoro katika Manispaa ya Ilemela, akidaiwa kumuua mtoto wa mwajiri wake Kelvin Kastus mwenye umri wa miezi 11 kwa kumziba pumzi.

Ameeleza kuwa, mtuhumiwa alitenda kosa hilo kwa kutumia shuka na kusababisha kifo chake, na sasa wanaendelea na upelelezi kubaini chanzo cha mauaji hayo mara utakapokamilika atafikishwa mahakamani.

Ata hivyo, Kamanda huyo wa Polisi amewataka wazazi na walezi wenye watoto wadogo kujenga utamaduni wa kuajiri watu wanaowafahamu kwa tabia, mienendo na malezi yao kwa sababu kuwaachia watu wasiowafahamu vizuri kazi ya kuwalelea watoto wadogo ni hatari.