May 15, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

CCM: WATENDAJI WA SERIKALI WATUMIKIE WANANCHI

Na Joyce Kasiki,Timesmajira,Online

CHAMA Cha Mapinduzi  kimewataka Viongozi na Watendaji katika ngazi mbalimbali za Serikali washughulike kutatua kero na changamoto zinazowakabili Wananchi katika maeneo yao, pamoja na kusimamia haki na kupinga aina zote za dhuluma na uonevu kwa wananchi.

Chama kimesisitiza kuwa mtumishi atakayeshindwa kutekeleza maagizo hayo anahatarisha ajira na nafasi yake ndani ya Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Msimamo huo wa Chama na maelekezo yametolewa leo na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Daniel Chongolo akihutubia wanachama wa CCM katika Ofisi za Chama Mkoa wa Dodoma, amesema CCM na Serikali imepania kuharakisha maendeleo ya watanzania kwa kasi na ufanisi mkubwa.

Chongolo amesema Rais Samia anafanya juhudi  kubwa za kujenga na kuimarisha mahusiano ya ndani na nje ambayo yatachochea ukuaji wa  sekta za biashara, kuvutia uwekezaji, kuondosha vikwazo na urasimu mipakani na kutoa fursa kwa Wananchi kujiajiri na kujiongezea kipato
kwa manufaa yao na Taifa. 

“Rais anahimiza ukusanyaji wa kodi na kusisitiza kila mfanyabiashara kulipa kodi kwa wakati na usahihi. Amesisitiza wakati wote kuwa Mamlaka za ukusanyaji kodi kutoza kodi kwa viwango stahiki na kwa haki lengo likiwa kuwezesha wafanyabiashara  wakuze mitaji yao na kupata faida halali ya biashara wanazofanya. Ni muhimu watendaji wenye dhamana wakaelewa  dhima na mwelekeo huo wa Kiongozi wetu wa Chama na Serikali” amesema Chongolo.

Katibu Mkuu huyo wa CCM amesema kuwa Wananchi wa Tanzania wanatambua umuhimu  wa kutunza amani, na kuendeleza umoja, mshikamano na Utulivu. Hali ya amani na usalama inaimarisha na kuongeza ari katika uwekezaji na kuzidisha juhudi katika uzalishaji mali lakini pia Wananchi kuishi katika furaha na hivyo kupata maendeleo.

“Hivi karibuni Rais aliwatumia ujumbe wale wachache wasio na uzalendo, wanaojaribu kufanya vitendo vya kuvunja sheria za nchi kuwa wasijaribu kwani dola iko macho. Ameonya watu hao kuacha mara moja kushiriki vitendo vya uhalifu na ujambazi. Waache kupima kina cha maji kwa miguu kwani watatumbukia kwenye mikono ya sheria” ameeleza Chongolo.

Chongolo amesema Mkuu  wa Nchi hayupo tayari kuona watanzania wakibugudhiwa na  makundi ya watu wenye nia ovu, wanaotaka kutajirika kwa njia za unyang’anyi, uporaji au kushiriki vitendo vya ubadhirifu ,ufisadi na ukwapuzi wa mali za umma.

“Wanaodhani Nchi yetu ni shamba lisilo mwenyewe waondoke fikra hizo.Wasidhani kama wanaweza kujifanyia wanavyotaka. Nchi yetu inaonozwa kwa mujibu wa  sheria .Hatachekewa mtu yeyote aidha kwa wizi wake , ubadhirifu wa fedha za miradi ya umma na kukwepa kulipa kodi “Amesema 

Hata hivyo  Chongolo amesjsitiza chama cha Mapinduzi kitakwenda sambamba na watendaji wasioohesha nia ya kuwatumikia wananchi nchi ina  watu  wengi ambao wanahitaji ajira hivyo kuondolewa kwa watendaji wazembe na kuwekwa wengine si kazi ngumu