April 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

“BUSH MEAL”zao jipya la utalii pori la akiba kijereshi

Na Mwandishi wetu

UBUNIFU wa mbinu za kuongeza idadi ya watalii na vyanzo vya mapato nchini kwa kuanzisha mazao mapya ya utalii ni mojawapo ya mikakati inayopigiwa chapuo kwa msisitizo mkubwa na Wizara ya Maliasili na Utalii chini ya Waziri mwenye dhamana ya Maliasili Angellah Kairuki.

Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania – TAWA kupitia Hifadhi ya Kijereshi iliyopo wilaya za Busega na Bariadi Mkoani Simiyu imetumia vyema fursa hiyo kubuni aina mpya ya zao hilo la utalii.

Zao hilo jipya linatoa fursa kwa watalii kula chakula Hifadhini “Bush Meal” huku wakitazama na kufurahia mazingira tulivu na vivutio mbalimbali vilivyopo ikiwa ni pamoja na kubarizi katika pepo zivumazo zenye kutoa hewa mwanana, mambo yanayomfanya mgeni afurahie muda wake alioutumia na fedha aliyoitoa kutalii katika hifadhi husika.

Aina hii ya utalii imeonekana kuwavutia wageni wengi katika hifadhi hiyo ambapo Februari 12, 2024 Kijereshi ilipokoea watalii kutoka Uingereza kwa ajili ya kufanya aina hiyo ya utalii ambapo muda wote walionekana kuufurahia ikizingatiwa kuwa Hifadhi ya Kijereshi inatambulika kama “Kiota cha Mbuni” (The Nest of Ostrich) katika ikolojia ya Serengeti Masai Mara kwa kuwa na idadi kubwa ya ndege nyuni aina ya mbuni wanaoipamba hifadhi hiyo.

TAWA inaendelea kuwaalika watanzania wote kutembelea na Kutalii Katika Hifadhi hiyo na Hifadhi nyingine nyingi zilizo chini ya Mamlaka hiyo kwa ajili ya shughuli za utalii.