May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Bukoba yatwaa tuzo anwani za makazi

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online,Bukoba

MANISPAA ya Bukoba Mkoani Kagera imepokea tuzo ya kutekeleza kwa ufanisi mradi wa anwani za makazi kwa kutumia fedha za ndani licha ya kuwa haikuwa kwenye mpango wa halmashauri zinazotekeleza mradi huo.

Mkurugenzi msaidizi Wizara ujenzi Uchukuzi na mawasiliano Carolin Kanuth Kulia akimkabithi Tuzo Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba Japhet Kanoni,kwenye hafla ya kukabithi Tuzo hizo zilizotolewa na wizara hiyo.Mpigapicha Wetu

Taarifa iliyotolewa na mkurugenzi msaidizi huduma za posta kutoka Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano Carolini Kanuth mjini Bukoba, amesema kuwa kufuatia kongamano lililofanywa na wizara hiyo waliamua kutoa tuzo kwa halmashauri ambazo zimetekeleza kwa ufanisi mradi huo.

Amesema kuwa zilichaguliwa manispaa mbili ikiwemo moja kutoka jiji la Mwanza ambapo ameeleza Manispaa ya Bukoba walianza kutekeleza mradi huo baada ya kupata mafunzo bila kusuburi pesa kutoka sehemu nyingine.

Ameelezea umuhimu wa mradi huo kwa jamii,katibu tawala wa mkoa wa Kagera Prof. Faustine Kamuzora ambaye ni muasisi wa mradi huo, amesema kuwa anwani za makazi zinarahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Kamuzora ameongeza kuwa uwepo wa namba kwenye nyumba pamoja na majina ya barabara na mitaa urahisisha huduma mbalimbali kama huduma za zima moto pale ajali hizo zinapotokea

Akielezea mpango uliopo kwa sasa,kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba Japhet Kanoni amesema kuwa kwa mwaka 2020 na 2021, wametenga kiasi cha shilingi milioni 45 baada ya zoezi la majaribio la kuweka namba na vibao vya majina ya mitaa kufanikiwa.

Mpaka sasa katika Manispaa ya Bukoba tayari barabara 100 zimetambuliwa kwa kuwekewa vibao zikiwemo nyumba 49.