May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Bodi ya nyama yawatoa hofu wananchi ulaji wa nyama,yatoa maelekezo

Na Zena Mohamed,TimesMajiraOnline,Dodoma

BODI ya Nyama Tanzania,imewatoa hofu wananchi kuhusu mkanganyiko wa baadhi ya watu kusema nyama ni mbaya kwa binadamu nakusema kuwa kuwa mbaya au nzuri nikutokana na kiasi unachokula na aina ya nyama unayokula.

Kauli hiyo imetolewa jijini hapa leo na Msajili wa Bodi hiyo,Dkt.Daniel Mushi wakati akizungumza na waandishi wa habari  kuhusu utekelezaji wa majukumu ya bodi ya nyama Tanzania kwa mwaka wa fedha 2022-2023.

Dkt. Mushi ameeleza ili mwili wa binadamu upate virutubisho vyote muhimu mtu mmoja anatakiwa kwa wiki walau ale kilo moja ya nyama kwani virutubisho vinavyopatikana kwenye nyama nyekundu havipatikani kwenye mimea na kitaalamu mtu anapaswa kula nyama angalau kilo hamsini kwa mwaka.

“Lakini kuna baadhi ya watu wamekua wakisema nyama ni mbaya kwa binadamu lakini niwambie uzuri wa nyama au ubaya   wa kula nyama unatokana na kiasi cha nyama mtu anachokula na aina ya nyama anayokula,”ameeleza.

Amefafanua kuwa endapo mtu atakula nyama kwa kiwango kinachotakiwa mtu huyo atakua na afya kwani itasaidia kuimarisha kinga ya mwili yakupambana na magonjwa nyemelezi na nguvu yakufanya kazi hivyo itasaidia kuongeza uzalishaji.

“Kama mnavyo fahamu nyama ndio njia rahisi ya kuondokana na utapia mlo,mtu anapowaambia watanzania wasile nyama nadhani haelewi vizuri hali ilivyo katika ulaji wa nyama na sisi kama Serikali tunampango wa kuhamasisha watanzania wale nyama hasa wanawake lakini ulaji nyama uliosahihi,”amesema.

Hata hivyo amesema bodi hiyo inajukumu la kukikisha kuwa inalinda afya ya mlaji kupitia udhibiti na ukaguzi sambamba na kuhamasisha uzajishaji bora wa nyama ili kupata masoko nje ya nchi.

“Kwasasa mtanzania mmoja anakula nyama takribani kilo 15 kwa mwaka kuanzia januari mpaka disemba lakini tunapaswa kula nyama angalau kilo 50 kwa mwaka kwa wenzetu Ulaya wanakula mpaka kilo 100 mtu mmoja kwa mwaka,

Sasa unapokuwa nyama kiasi kinachotakiwa kwanza unakuwa na afya unakuwa na nguvu ya kufanya kazi na uzalishaji unaongezeka lakini pia unakuwa na uwezo wa kinga ya mwili kuweza kujikinga na magonjwa kinga zinakuwa Imara,”amesema.