May 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri Mkuu wa Israel, Naftali Bennett. (Picha na GettyImages).

Bennett amrithi Netanyahu nchini Israel

TELAVIV, Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu ameondolewa madarakani baada ya Bunge la Taifa la Knesset kupiga kura ya kuidhinisha serikali mpya ya muungano chini ya Naftali Bennett.

Netanyahu kupitia Chama cha Likud alihudumu kwa miaka 15 katika nafasi hiyo kutoka 2009 hadi 2021 na hapo awali kutoka 1996 hadi 1999.

Aidha, Bennett kutoka mrengo wa kulia tayari ameapishwa rasmi kuwa Waziri Mkuu wa Israel ambaye anachukua nafasi.

Bennett ambaye ana umri wa miaka 49 ni mwanasiasa wa Israel ambaye anatajwa kuwa na nafasi kubwa ya kuendelea kuliongoza Taifa hilo na anakuwa Waziri Mkuu wa 13 kuanzia Juni 13, 2021 kupitia Chama cha Yamina.

Awali alihudumu kama Waziri wa Mambo ya Diaspora kati ya mwaka 2013 hadi 2019 na mwaka 2019 hadi 2020 alihudumu kama Waziri wa Ulinzi nchini Israel.

Bennett kwa sasa ataongoza muungano wa vyama ulioidhinishwa kupitia uongozi mwembamba wa walio wengi wa 60 kwa 59 ambapo atahudumu kwa miaka miwili na nusu kuanzia sasa hadi Septemba 2023.

Kupitia makubalino yao atamkabidhi nafasi hiyo ya Uwaziri Mkuu, Yair Lapid ambaye ni kiongozi wa chama cha mrengo wa kati cha Yesh Atid, kuongoza kwa miaka mingine miwili.

Netanyahu anaondoka akiwa na historia ndefu ya kuhudumu kwa miaka mingi kwa nafasi hiyo na kukabiliwa na mashtaka ya uhalifu akiwa madarakani huku akishindwa kujinasua katika tuhuma mbalimbali zikiwemo za kifisadi.

Pia anaondoka baada ya kushindwa kufikia mwafaka katika chaguzi nne mfululizo ambazo zilianza kufanyika mwaka 2019,akashindwa kupata uungwaji mkono wa kutosha ili kuunda serikali mpya ya muungano huku zikifuatia chaguzi zingine mbili ambazo zilifanyika bila mafanikio

Aidha, Disemba, mwaka jana ukafanyika uchaguzi wa nne ambapo licha ya ukubwa wa chama chake cha Likud katika Bunge la Taifa ambalo linaudwa na viti 120, malengo yake ya kuunda Serikali yalishindikana, hivyo Yair Lapid ambaye chama chake cha mrengo wa kati cha Yesh Atid kilikuwa cha pili kwa ukubwa akapewa nafasi.

Tangu awali upinzani uliokuwa ukipinga utawala wa Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu madarakani uliongezeka hata kwa vyama vyenye msimamo sawa na chake.