April 28, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Azaki zaungana kutoa msimamo wa pamoja katika mkutano wa COP27

Na Mwandishi wetu,timesmajira

AZAKI  mbalimbali nchini zimeungana na kutoa msimamo wa pamoja kuelekea Mkutano wa kimataifa wa COP 27 dhidi ya mabadiliko ya Tabianchi  kusisitiza utoaji wa fedha kuhakikisha uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kupata nafuu na ahueni kutokana na hasara na uharibifu unaosababishwa na majanga yanayochagizwa na mabadiliko ya tabianchi. 

Taarifa iliyotolewa na Azaki hizo hivi karibuni imesema wanahitaji mifumo na michakato ya kuwezesha upatikanaji wa fedha hizi kuwekwa vizuri na kuhakikisha upatikanaji wa moja kwa moja wa fedha hizi.

Ilisema kuwa azaki hizo zinasisitiza udhibiti wa uzalishaji wa gesi joto kwa nchi zilizoendelea kwa kuongeza nia zao pamoja na kuwezesha ufyonzaji wa gesi joto, ili kupunguza madhara na athari za mabadiliko ya tabianchi.” Uharibifu na upoteaji wa mali inayosababishwa na athari za mabadiliko ya tabianchi, 

pamoja na kuhimiza ukamilishaji wa mkataba wa Paris,”imesema na kuongeza 

“Tunakataza ushawishi na uletaji wa nyenzo, teknolojia na suluhisho zenye lebo ya ukabilianaji na athari za mabadiliko ya tabianchi ambazo ni za uongo zisizo na tija katika utunzaji wa mazingira,zinazodidimiza maendeleo na zinazo jenga utegemezi kwa nchi zinazoendelea na kukataza siasa chafu zenye lengo la kuchelewesha utekelezaji wa mkataba wa Paris na zenye kunufaisha wazalishaji wakubwa wa gesi joto katika mkutano huu,”imesema.

Aidha imesema  wanasisitiza kuangalia zaidi masuala yatakayoongeza ustahimilivu na udhibiti wa mabadiliko ya tabianchi na kuhitaji wa kujengewa uwezo na kupatiwa teknolojia ili kuwezesha ustahimilivu wa mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuwezesha hatua shahiki za kupunguza athari na uharibifu  unaochagizwa na mabadiliko ya tabianchi.

Pia imesema kuwa wanahitaji wawakilishi kutoka Afrika na kwenye makundi ya pamoja kuwa na umoja na kusimamia hoja za msingi za maendeleo ambazo zinazingatia uwezo na haja za jamii zilizo na mazingira magumu kustahimili athari za mabadiliko ya tabianchi.

“Tunasikitishwa na upungufu wa kila mwaka wa uwakilishi na ushiriki wa azaki na wawakilishi wa jamii katika Mikutano hii, kupitia utoaji wa nafasi chache za ushiriki, uzuiaji wa kushiriki ndani ya vyumba vya mkutano na vikwazo vingi kwenye utoaji visa kwa wenyeji wa mikutano,”Imesema .