May 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Atuhumiwa kuiba mtoto,kumridhisha mme wake

Judith Ferdinand,TimesMajira Online, Mwanza

Mwanamke mmoja aliyetambulika kwa jina la Sara Robert,mwenye umri wa miaka 33,Mkazi wa Sengerema anashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza kwa tuhuma za kuhusika na wizi wa mtoto wa miezi mitatu.

Ambapo lengo la mwanamke huyo kumuiba mtoto huyo mwenye jinsi ya kiume ilikuwa ni kumridhisha mme wake ambaye alikuwa anataka mtoto wa kiume baada ya watoto waliobahatika kuwa nao wakiwa ni wa jinsi ya kike tu.

Akizungumza jijini hapa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa, ameeleza kuwa katika tukio hilo lilitokea Januari 14,2023 majira ya saa 2(20:00 ) usiku huko maeneo ya Kitongoji cha Nyankololo, Kijiji cha Nyamtelela, Tarafa na Wilaya ya Sengerema.

Ambapo iliripotiwa taarifa ya kuibiwa kwa mtoto wa kiume mwenye umri wa miezi mitatu na mtu/watu wasiojulikana.

Ameeleza kuwa baada ya taarifa hizo kuripotiwa kituo cha Polisi, Askari walianza ufuatiliaji nailipofika Aprili 08,2023 walifanikiwa kumkamata Sara Robert (33),mkulima, mkazi wa Nyashitale akiwa na mtoto huyo ambapo mama mzazi wa mtoto huyo aliweza kumtambua kuwa ndiye aliyekuwa ameibwa.

“Baada ya mahojiano ya kina, Sara Robert alikiri kuhusika na wizi wa mtoto huyo na kudaikuwa alitaka kwenda kumridhisha mume wake kwa kumhadaa kuwa amepata mtoto wa kiume kwani watoto aliobahatika kuwa nao wote ni wakike na afya ya mtoto inaendelea vizuri,”ameeleza Mutafungwa.

Pia ameeleza kuwa pamoja na uchunguzi mwingine umefanyika na amekabidhiwa kwa wazazi wake kwa malezi,mtuhumiwa atafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo mara baada ya kukamilishwa kwa upelelezi.