May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkuu wa Wilaya ya Singida Mhandisi Paskasi Muragili akiwasisitiza wafanyabiashara wadogo juu ya matumizi sahihi ya vitakasa mikono alipofanya Operesheni maalum ya Tokomeza Corona Katika Manispaa ya Singida kwenye Soko Kuu la Singida Mjini. (Picha ya Mtandao).

Atozwa 50,000/- kwa kukiuka masharti ya kujikinga na Corona

Na Damiano Mkumbo, Singida

Serikali Wilayani Singida imeanza operesheni maalumu ya kuwakamata na kuwatoza faini ya shilingi 50,000/= papo kwa papo watu wasiyotekeleza masharti ya kujikinga dhidi ya ugonjwa wa Corona COVID-19.

Hatua hiyo inayongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Singida, Paskal Muragili imemnasa mhudumu moja wa duka la vifaa vya bajaji na bodaboda lililopo mtaa wa zamani kona ya kuelekea soko la Msufini Fanuel Aroni, kwa kutoa huduma bila kunawa mikono ingawa vifaa vimewekwa mbele ya duka hilo.

Mhudumu wa duka hilo ametozwa faini ya shilingi 50,000 papo hapo au biashara hiyo kufungwa kwa kukiuka maagizo ya serikali juu ya masharti kujikinga dhidi ya ugonjwa wa Corona uliyolipuka duniani.

Akizungumza na Majira jana mchana baada ya kukagua duka hilo Mkuu wa Wilaya ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, alisema watu wamekuwa na mwitikio mkubwa wa kutekeleza agizo hilo, lakini bado wengine wamekuwa na tabia ya kutozingatia kwa vitendo kuhakikisha wananawa mikono kabla na baada ya huduma.

“Kwa kushirikiana na wataalamu wa afya na biashara, pamoja na Jeshi la Polisi operesheni hiyo iliyoanza siku ya Jumatatu wiki hii tumeanza kuchukua hatua kali ikiwa ni pamoja na kufunga biashara na huduma za watu ambao wanakiuka maagizo hayo ya kujinusuru na ugonjwa huo” alisema Muragili

“Hatua nyingine tuliyochukua ni kupima joto wageni wote wanaoingia katika mji wa Singida kutoka mikoa mingine na nje ya nchi, kwa kutumia vifaa vitano vya Thermo scaner kimoja kikiwa kimewekwa kituo cha mabasi cha Misuna mjini hapo katika hatua za awali, wale ambao wanaoonekana na hali ya kawaida wanaendelea na safari zao” alisema