May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RUWASA:Asilimia 77 ya wananchi vijijini wafikiwa na huduma ya maji

Na Joyce Kasiki,Timesmajira online,Ruangwa

KATIKA kipindi cha miaka minne tangu kuanzishwa kwa Wakala wa  Huduma ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) ,asilimia 77 ya wananchi waishio vijijini wamefikiwa na huduma hiyo.

Akizungumza katika maonyesho ya Kimataifa ya Madini yanayofanyika katika wilaya ya Ruangwa  mkoani Lindi,Meneja  Uhusiano na Masoko RUWASA Makao Makuu Athuman Sharrif amesema,lengo ni kufika asilimia Zaidi ya 85 ya upatikanaji huduma ya maji vijijini ifikapo 2030.

“Kama mnavyofahamu RUWASA  ilianza kazi rasmi 2019 ambapo sekta ndogo ya maji viijini tuliikuta ina wastani wa huduma kwa asilimia 64.8, lakini mpoka leo kwa kipindi cha miaka minne tangu kuanzishwa kwa RUWASA tumefikia asilimia 77.”amesema na kuongeza kuwa

 “Kwa hiyo kwa kipindi cha miaka miwili hatuna wasiwasi tunaweza kufika kabisa zaidi ya asilimia 85 na zaidi ,lakini maelekezo ya serikali na chama tawala inatutaka ifikapo 2025 tuwe tumefikia wastani wa huduma ya maji vjijini kwa asilimia zaidi ya 85 na ifikapo 2030 tuhakikishe kila kijiji, kila kitongoji Tanzania Bara kinapata huduma ya mani safi salama na yenye kutosheleza “

Ameongeza kuwa “Na kama mnavyofahamu Tanzania tuna vijiji zaidi  11,587 kati ya  vijiji 12,319 vilivyopo,na katika vijiji hivyo RUWASA inahudumia vijiji 11,587 nambapo kati ya hivyo tayari tumeshafikia na kuvipa huduma ya maji safi salama na yenye kutosheleza vijiji 9,670 ,kwa hiyo hapo utaona tuna wastani wa vijiji 1,918 tu ndiyo bado hatujavifikia kwa huduma ya maji safi salama na yenye kutosheleza.”

Hata hivyo amesema katika kuhakikisha huduma za upatikanaji maji safi,salama na yenye kutosheleza inapatikana kwa uhakika,Rais Samia Suluhu Hassan amenunua mtambo mmoja wa kuchimba kisima kila mkoa Tanzania bara kasoro mkoa wa Dar es Salaam huku akisema mtambo huo una ufanisi mkubwa wa uchimbaji wa kisima kirefu zaidi ya mita 200 kwenda chini.

“Hizi nyezo hazikuwepo hapo awali,kwa hiyo sasa kasi ni kubwa na ili maji yapatikanae ni lazima kuwe na chanzo cha maji cha uhakika,hivyo kasi ya upatikanaji wa huduma ya maji itaongezeka hata hapa mkoa wa Lindi katika wilaya zake tatu ikiwemo ya Ruangwa ambapo kuna mradi unatekelezwa na RUWASA ambao utanufaisha Zaidi ya vijiji 56 .”amesema Sharrif

Ametumia nafsi hiyo kuwaondoa wasiwasi wananchi hasa waishio vijijini pamoja na wawekezaji wa madini na uwekezaji wowote ,waende maeneo ya vijiji na tayari utaratibu mzuri upo na kama hakuna huduma yoyote ya maji lakini RUWASA katika maeneo husika wana majibu ya nini kinafanyika katika eneo huska ili kupata maji.

“Kwa hiyo wawekezaji wasiwe na mashaka ,wasiwe na wasiwasi tunawakaribisha maeneo ya vijijini kwa sababu serikali imeunda wakala huu ili kuihakikisha maeneo yote ya vijijini yanapata huduma ya maji safi salama na yenye kutosheleza.”amesisitiza Sharrif

 Kuhusu ushiriki wao kwenye maonyesho hayo ya madini Sharrif amesema,wameshiriki katika maonyesho hayo ya uwekezaji na madini mkoani Lindi kwa sababu sekta ya maji ni muhimu sana katika uwekezaji wa sekta ya madini na kwamba maji yanahitajika ili kuwezesha shughuli hiyo kufanyika kwa ufanisi.