October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Prof.Lipumba ajitosa tena kugombea urais

Na Irene Clemence

MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba amechukua fomu ya kuomba ridhaa ya chama chake kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba mwaka huu.

Profesa Ibrahim Lipumba amechukua fomu baada ya kuridhia ombi la Jumuiya ya Vijana ya CUF (JUVCUF) Mkoa wa Dar es Salaam ambao walimchukulia fomu kwa ajili ya kugombea nafasi ya urasi kupitia Chama hicho.

Akizungumza Jijini Dar es salaam jana wakati wa kumkabidhi fomu hiyo Profesa Lipumba, Katibu wa Jumuiya ya Vijana JUVCUF wilaya ya Ilala, Salim Muslim alisema vijana hao wameamua kumchukulia fomu kutokana na kuguswa na itikadi ya furaha kwa wote ambayo imekuwa ikitekelezwa na chama hicho.

Alisema wagombea wote waliojitokeza kuomba ridhaa ya kugombea urais kupitia Chama hicho waliwapima kwa sera zao na kuona ni vema kumshawishi Profesa Ibrahim kuchukua fomu kwani anaweza Kupambana na wagombea wengine wa upizani ambao wanagombea nafasi hiyo.

“Sisi kama vijana tumeugana pamoja na kuamua kuchangishana fedha kwa lengo la kumchukulia fomu Profesa Lipumba tuna imani ataweza kutimiza adhima ya haki sawa kwa wote,”alisema Muslim.

Naye Mwenyekiti wa Chama hicho Profesa Ibrahim Lipumba aliwapogeza vijana hao kwa uamuzi mkubwa walioufanya kwani ni mkubwa na unapaswa kuigwa na watu wengine.

Profesa Lipumba alisema aliamua kutokuchukua fomu awali wakati zoezi hilo lilipoanza ili kutoa nafasi kwa watu wengine kujitokeza kugombea nafasi ya Urais.

“Nilisita kuchukua fomu awali ya kugombea urais kupitia Chama hichi ili kutoa fursa kwa wanachama wengine kuchukua fomu kugombea uongozi.

“Nashukuru sana vijana hawa kuamua kunishawishi kwa kunichukulia fomu,”alisema Profesa Lipumba. Aidha Profesa Lipumba alisema chama hicho kikipata ridhaa ya kuogoza nchi kitaunda serikali ya umoja wa kitaifa kwa lengo la kukabiliana na matatizo sambamba na kujenga mfumo wa kutatua matatizo.

Pia alisema chama hicho kitahakikisha kinasimamia itikadi ya furaha kwa wote kwa kuhakikisha kila kijana na watoto wanapata afya bora .