October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Wachezaji Yanga wavuna ‘mkwanja wa maana’, GSM, Viongozi wafufua mikakati ya Ubingwa FA

Na Mwandishi Wetu

BAADA ya kupata ushindi wa 2-1 dhidi ya Kagera Sugar ulioiwezesha timu ya Yanga kutinga hatua ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam (Azam Sports Federation Cup) wachezaji wa timu hiyo wamebeba kitita cha Sh. milioni 36 kutoka kwa mdhamini GSM na Kamati ya Mashindano.

Katika mchezo huo, Kagera walikuwa wa kwanza kupata goli dakika ya 20 lililofungwa na kiungo Awesu Awesu kabla ya David Molinga kufunga goli la kusawazisha dakika ya 52 kwa kichwa huku Deus Kaseke akifunga goli la ushindi kwa mkwaju wa penalti dakika ya 76.

Kwa mujibu wa viongozi wa Yanga wamesema kuwa, fedha hizo ni ahadi kutoka kwa mdhamini wao GSM aliyeahidi kutoa milioni 30 huku Kamati ya Mashindano na wadau wake wakichangia Sh. milioni 6.

Mbali na fedha hizo kutoka kwa viongozi lakini pia matawi mbalimbali yamechanga na yanaendelea kuchanga fedha ambazo watapeleka kwa wachezaji kama sehemu ya kuwapa motisha katika mechi yao ijayo ya nusu fainali ambayo watavaana na Simba.

Mmoja wa kiongozi ambaye hakutaka jina lake kutajwa amesema, kabla ya mchezo huo, GSM kupitia godoro la GSM Foam iliahidi zawadi hiyo endapo timu itafanikiwa kusonga mbele lakini pia iliahindi nyongeza endapo timu ingelipa kisasi kwa kupata ushindi wa mabao matatu na zaidi

Amesema ,wao kama viongozi ushindi huo sasa umefufu morali kubwa zaidi ya kuandaa mikakati imara itakayowawezesha kutwaa kombe hilo ili kurudi katika mashindano ya kimataifa.

Toka awali mara baada ya kutokuwepo na dalili za kuweza kutwaa Kombe la Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL) msimu huu, walianza kufufua harakati zao za kuhakikisha wanahamishia nguvu katika michuano ya Kombe la Shirikisho la Azam.

Pia viongozi hao pamoja na wadhamini wao, GSM, walikaa vikao maalum kadhaa na wachezaji ikiwa ni maandalizi ya kurejea kwa morali ya hali ya juu ili kufika fainali katika mashindano hayo.

Amesema, hata walipokuwa katika maadalizi ya mwisho kuelekea kwenye mchezo huo wa juzi, ahadi ya wachezaji ilikuwa ni kupambana ili kusonga mbele kwani wanachotaka ni ushiriki wenye tija katika mashindano hayo na ndio maana ilikuwa ni lazima wapename mikakati mapema ili kila mchezaji na kiongozi ajue wajibu wake atakaopaswa kuutekeleza kikamilifu

Hata hivyo baada ya mchezo huo, kocha mkuu wa Yanga, Luc Eymael aliwapongeza wachezaji wake kwa mchezo mzuri waliouonesha na walistahili kushinda.

“Katika mchezo wetu malengo yalikuwa ni nkushinda na kusonga katika hatua inayofuata na tunashukuru hili limewezekana hivyo nawapongeza sana wachezaji wangu kwa uwezo waliouonesha, ” amesema Eymael.

Aidha alieleza kuridhishwa kwake na kiwango kilichooneshwa na mshambuliaji wao David Molinga ambaye amekuwa na kiwango bora katika mechi kadhaa za Ligi Kuu zilizopita.

Amesema, licha ya kuwa bado kuna mambo hayapo sawa kwa mchezaji huyo ikiwemo kupunguza uzito lakini mara kadhaa amewaokoa na kuwapa pointi kwenye michezo muhimu.

Kuhusu Winga Benard Morrison, kocha huyo amesema kuwa kwa sasa jambo hilo lipo kwa viongozi wa klabu hivyo wanachosubiri ni tamko litakalotolewa na viongozi.

Siku chache zilizopita Morrison ameripotiwa kuwa na mgogoro na viongozi wa klabu yake hasa kutokana na sintofahamu ya mkataba wake huku pia akiripotiwa kuonesha tabia zisizofaa.

Kocha huyo amesema baada ya kuona aelewi tabia za utovu wa nidhamu za mchezaji huyo alilazimika kuondoa kikosini na kambo hilo likukabidhi rasmi kwa viongozi.