April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Chongolo ataka miradi ya maendeleo kuzingatia thamani ya fedha

Na Mwandishi wetu,Timesmajira Online

CHAMA Cha Mapinduzi kimemuagiza mkuu wa mkoa wa Rukwa

Joseph Mkirikiti kuunda kikosi kazi cha kukagua na

kufanya tathmini ya miradi inayotekelezwa mkoani humo

ili kujua ikiwa utekelezaji wake unakidhi thamani ya

fedha zilizotumika.

Kimebainisha kuwa hakikuridhishwa na miradi

walioitembelea hasa katika sekta ya afya ambayo

inayokabiliwa na changamoto kubwa ya dawa, wataalam,

huduma duni kwa wazee pamoja na maeneo mengine kuwa

na utekelezaji wa miradi isiyoendana na thamani ya

fedha iliyotumika

Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa chama hicho Ndugu

Daniel Chongolo katika kikao cha majumuisho ya ziara

yake ya siku mbili mkoani humo, iliyoambatana na

wajumbe wa Sekretarieti ya Halmashauri kuu ya CCM

Taifa, kilichofanyika ukumbi wa mikutano manispaa ya

Sumbawanga.

“Naagiza na kukuelekeza mkuu wa mkoa uunde timu ya

wataalam kwa ajili ya kukagua na kufanya tathmini ya

miradi yote inayotekelezwa mkoani kwako ili kujua hali

halisi ya kinachoendelea hususani kwenye eneo la

thamani ya fedha zilizotumika hapa, mambo hayaendi

vizuri kabisa” Amesema Chongolo.

Amefahamisha kuwa CCM haiko tayari kuwalea viongozi na

watendaji wazembe wanaoonekana kushindwa kutatua kero

za wananchi na kuimarisha ustawi wao, hivyo kati siku

14 atahitaji kupata ripoti ya utekelezaji wa maelekezo

hayo na hatua kali zichukuliwe itakapobainika kuna

ubadhirifu ama uzembe ambao unakwambisha ufanisi wa

miradi hiyo.

“Nahimiza watendaji wa serikali kuwa waadilifu kwa

kuheshimu fedha za umma. Hakikisheni fedha zinazoletwa

au kutengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo

zinatafsirika kwa wananchi kwa kuwaletea unafuu na

kuimarisha huduma za kijamii na kiuchumi kwao.”

Amesema Chongolo.

Hata hivyo, Chongolo amesema atakaporejea Dodoma

watawaita mawaziri wanaohusika na sekta za afya, maji,

ardhi na Tamisemi ili kujiridhisha juu ya mipango yao

na kujua mkwamo ama urasimu unatokea katika eneo gani

na kupelekea huduma kusuasua na kuwa sio za kiwango

cha ufanisi kwa wananchi.

“Tunataka watueleze nani anasababisha mkwamo katika

upatikanaji wa huduma, nasema hivi nikitambua sisi

viongozi tunawajibu wa kufuatilia na kusimamia,

tutakuwa wakali, ni lazima tuogope fedha ya umma,

ukizitumia vizuri zitakujengea heshima, ukizitumia

vibaya zitakuvunjia heshima kwa wananchi, hivyo kila

mmoja anapaswa kuwa mwadilifu katika kusimama dhamana

aliyopewa,” Amesema Chongolo

Amesema, kila kiongozi na mtendaji katika chama na

serikali anawajibu wa kutimiza wajibu wake kwa

kuhakikisha upatikanaji wa tija huduma za kijamii

unakuwepo kama anavyosisitiza Rais Samia Suluhu

Hassan wakati wote.